Iweni ni vyombo vya Injili ya matumaini kwa Watu wa Mungu
Watawa wanahamasishwa na Mama Kanisa wakati huu kutoka ili kuuona ukweli wa mambo
badala ya kujifungia katika nyumba zao za kitawa; wanapaswa kutoka ili kusikiliza
na kujibu kilio cha damu pamoja na mahangaiko ya watu wanaowazunguka; wanahimizwa
kutoka ili kuisindikiza Familia ya binadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani,
kwa kutambua kwamba, wao kama watawa wanapaswa kuwa ni alama wazi ya Injili ya Matumaini
kwa Watu wa Mungu.
Haya ndiyo
yaliyojiri wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa hamsini na tatu wa wakuu wa Mashirika
ya Kitawa na Kazi za Kitume nchini Italia, uliohitimishwa hivi karibuni kwa kukutana
na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, aliyekazia pamoja na mambo mengine: umuhimu
wa kuonesha ushuhuda wa kinabii unaofumbatwa katika Mashauri ya Kiinjili, kama alivyofundisha
na kuishi Yesu mwenyewe kwa watu wa nyakati zake.
Watawa waoneshe mshikamano
wa udugu na upendo; wajenge moyo wa toba na wongofu wa ndani kwa kusimika maisha yao
katika Neno la Mungu, Sala na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, ili kuzungumza kwa
kina na Yesu anayejificha katika maumbo ya Mkate na Divai.
Mkutano wa wakuu
wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume uliokuwa unaongozwa na kauli mbiu “Utume
wa Kanisa na Maisha ya Kitawa mintarafu Waraka wa kichungaji uliotolewa na Baba Mtakatifu
Francisko, Injili ya Furaha. Maisha ya kitawa yanahitaji kwa namna ya pekee majiundo
endelevu yanayopyaishwa na upendo unaosimikwa katika mshikamano na maisha ya kidugu,
unaowawajibisha watawa kuwaendea wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana
na hali yao ya maisha: kiroho na kimwili. Lengo ni kuwaonjesha Injili ya Furaha na
Matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.
Watawa wanawajibika
kuwaendea watu ambao wanakabiliana na majanga katika maisha yao, ili kuwasikiliza
kwa makini, ili kuwaganga na kuwaponya; kuwapenda na kuwathamini; kuwaokoa na kuwaojesha
matumaini mapya. Watawa wanatambua ugumu na changamoto iliyoko mbele yao, lakini hata
hivyo bado wanathubutu kutoka kifua mbele ili kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili
ya Furaha.
Askofu mkuu Josè Rodrigues Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa
la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume, amekazia mambo makuu matatu: kwanza ni kwenda,
pili kuishi na tatu ni kuvuka mipaka. Watawa wawaendee watu ili kujenga umoja na mshikamano
wa kitawa, huku wakilitafakari Neno la Mungu na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa.
Watawa
waishi kwa kushuhudia ukweli unaojikita katika uwazi, upendo wa dhati pasi na unafiki,
majadiliano yanayoheshimu na kuthamini utu wa mtu; mang’amuzi mapana kwa kuonesha
utambulisho na mshikamano wao wa dhati unaowachangamotisha kujisadaka bila ya kujibakiza,
kwa ajili ya Mungu na jirani.
Watawa wajitambue kwamba, wao ni vyombo vya
haki, amani na upatanisho, daima wajitahidi kutafuta mafao ya wengi bila ya kujitafuta
na kujihurumia wenyewe. Watawa waoneshe moyo wa upendo na ukarimu kwa maskini na wote
wanaohitaji msaada wa hali na mali.
Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, akizungumza na Wakuu wa Mashirika ya kitawa na
kazi za kitume, amewataka watawa kuzama katika uhalisia wa maisha ya watu wanaowahudumia,
kwa kuwapokea jinsi walivyo na pale inapowezekana wajifunze kutoka kwao, kwa kuwashirikisha
utakatifu wa maisha unaotoa harufu yenye mvuto na mashiko katika huduma kwa maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Kwa njia hii anasema Askofu Galantino,
Mashirika ya kitawa na kazi za kitume yanaweza kuwa kweli, ni maabara ya binadamu
wapya, watu wenye uwezo wa kutoa maisha yao kwa ajili ya huduma kwa jirani zao bila
ya kujibakiza; kwa kuonesha moyo wa upendo na ukarimu; furaha na udugu. Maisha ya
kijumuiya hayana budi kujikita katika mshikamano wa kidugu na mapendo yanayomwilishwa
katika uhalisia wa maisha ya kila siku; kwa kuheshimu na kuzingatia karama na kanuni
za Shirika bila kumezwa na malimwengu, bali yote yawe ni kwa ajili ya sifa na utukufu
wa Mungu na binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Watawa wanahamasishwa
na Mama Kanisa kujifunza kwa bidii Waraka wa kitume wa Baba Mtakatifu Francisko ili
kuweza kuwahudumia watu kwa unyenyekevu, upole na mapendo makuu, kama kielelezo cha
Kanisa na wadau katika mchakato wa Uinjilishaji, kwa kuwahudumia na kuwaganga wale
waliovunjika moyo.
Watawa wawe na ujasiri wa kumwilisha karama xa mashirika
yao bila woga; kwa kushikamana na watu katika kumwilisha Mashauri ya Kiinjili; ili
watu waonjeshe huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Mashirika ya Kitawa na Kazi za
kitume. Watawa watambue kwamba, mtu jasiri anathubutu!
Na Padre Richard A.
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.