Kanisa linakazia: tunu msingi za maisha ya ndoa na familia na uhuru wa kuabudu!
Yaliyojiri katika maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia iliyofanyika
mjini Vatican kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014; maandalizi ya Siku ya Familia
Kimataifa itakayoadhimishwa katika Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani, mwaka 2015;
uhuru wa kidini na umuhimu wa Kanisa kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi
za maisha ya ndoa na familia ni kati ya mambo msingi yaliyojitokeza wakati wa mkutano
wa Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.
Maaskofu wamepembua mikakati ya kichungaji
kwa ajili ya mchakato wa Uinjilishaji mpya, kwa kujikita katika maadhimisho ya Ibada
na Ushuhuda wa imani tendaji, pamoja na kuwasaidia watu wanaoishi pembezoni mwa Jamii
kupata mafundisho ya Kanisa Katoliki.
Mkutano huu umefunguliwa kwa hotuba
iliyotolewa na Askofu mkuu Carlo Maria Vigano', Balozi wa Vatican nchini Marekani
aliyekazia umuhimu wa Kanisa kuendelea kutembea pamoja na Familia katika furaha, shida
na changamoto wanazokabiliana nazo kila siku, ili kwa kuonjeshwa huruma na upendo
unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, Familia ya binadamu iweze kuwa na matumaini
pamoja na kutekeleza dhamana na utume wake ndani ya Kanisa.
Ni wajibu wa Mama
Kanisa kuhakikisha kwamba, Familia zinaendelea kustawi katika imani, matumaini, mapendo
na mshikamano wa dhati; mambo msingi yanayoziwezesha kudumu, huku wakiwa wanaambatana
na Yesu Kristo kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Kanisa ni kielelezo cha huruma
na upendo wa Mungu; hapa anasema Baba Mtakatifu Francisko ni mahali ambapo waamini
wanaweza kujichotea huruma na kuonjeshwa ukarimu, upendo, msamaha pamoja na kuhamasishwa
kuishi maisha mema kadiri ya tunu msingi za Kiinjili.
Maaskofu Katoliki Marekani
wanasema, Famili za Kikristo hazina budi kufundwa mintarafu: Maandiko Matakatifu,
Mapokeo ya Kanisa pamoja na mang'amuzi ya wanandoa na familia bila kusahau mchango
unaotolewa na wachungaji wa Kanisa; ili kweli Familia ziweze kukabiliana na changamoto
zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na
teknolojia. Familia zinahamasishwa kusali na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa umoja,
ili kweli Familia ziweze kuwa ni Kanisa dogo la nyumbani.
Maaskofu wanasema,
Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa huko Philadelphia, itakua ni fursa kwa Mama
Kanisa kusikiliza, kuzungumza, kusali na kutafakari pamoja na wanandoa kutoka sehemu
mbali mbali za dunia, kwa matumaini ya uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko; ili kweli
Familia ziweze kuendelea kuwa ni wajumbe wa furaha na walinzi wa tunu msingi za maisha
ya ndoa na familia, kwa kung'ara zaidi na zaidi katika uaminifu kwa Injili ya Kristo.
Ni wajibu wa Familia kuendelea kutangaza Injili ya Uhai kwa kukataa kishawishi
cha kukumbatia utamaduni wa kifo, kama njia ya kulinda utu na heshima ya binadamu.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Marekani linamshukuru Mungu kwa kuwawezesha kwa njia ya mshikamano
wa upendo kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Furaha, hasa wale walioathirika kutokana
na majanga asilia na wale wanaoendelea kudhulumiwa na kunyanyaswa kutokana na imani
yao kwa Kristo na Kanisa lake. Mchakato wa Uinjilishaji maana yake ni kushuhudia imani,
matumaini na mapendo kwa Kristo na Kanisa lake, katika hali ya unyenyekevu, imara
na thabiti katika umoja na mshikamano.
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani
Mwaka 2015 litaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili
wa Vatican walipochapisha Tamko kuhusu uhuru wa kidini, yaani "Dignitatis Humanae";
msingi mkuu katika mahusiano kati ya watu; uhuru wa mtu kutenda kadiri ya imani yake
pamoja utume wa Kanisa katika masuala ya uhuru wa kuabudu. Huu utakuwa ni wakati muafaka
wa kufundisha umuhimu wa uhuru wa kidini pamoja na kuendelea kuinjilisha.
Ili
kukabiliana na changamoto, matatizo na fursa katika maisha ya ndoa na Familia, Maaskofu
hawana budi kutoka kifua mbele, kwa kufuata mfano wa Baba Mtakatifu Francisko ili
kujenga utamaduni wa watu kukutana, kwa kuwangoza kikamilifu wanandoa katika mapito
ya maisha kwa imani, matumaini na mapendo pamoja na kuendelea kukazia ushuhuda wa
tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.