Viongozi wa Serikali na nchi mbali mbali Barani Afrika, Jumanne tarehe 11 Novemba
2014 wameungana na mamillioni ya wananchi wa Zambia kumsindikiza Marehemu Rais Michael
Chilufya Sata katika usingizi wa amani. Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe anasema, Marehemu
Rais Sata alikuwa ni mtu wa watu, amefariki dunia huku akiwa na ndoto na mipango mikubwa
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Zambia, ambayo imebaki ikiwa imejikita
katika siri ya moyo wake!
Kifo cha Rais Sata ni pigo kubwa si tu kwa Zambia,
bali kwa Bara la Afrika kwa ujumla, kwani ni kiongozi aliyejifunga kibwebwe kupambana
na baa la umaskini miongoni mwa watu wake.
Katika Ibada ya pamoja kwa ajili
ya kumwombea Marehemu Rais Sata, iliyofanyika siku ya Jumatatu, tarehe 10 Novemba
2014 kwenye Ukumbi wa Bunge la Zambia, mjini Lusaka, viongozi mbali mbali wamewataka
wananchi wa Zambia katika ujumla wao, kuendelea kuwa na matumaini katika maisha ya
uzima wa milele, licha ya majonzi makubwa ambayo kwa sasa wanakabiliana nayo kwa kuondokewa
na mpendwa wao, ambaye viongozi wengi Kusini mwa Afrika walipenda kumwita "Sekuru".
Waamini wawe na imani katika ufufuko wa wafu kwani Yesu ameshinda mauti na kifo kwa
njia ya mateso, kifo na ufufuko wake pale Msalabani.
Waamini na viongozi kwa
namna ya pekee kabisa wamehamaishwa kukesha na kusali kwani hawajui siku wala saa
wanapoweza kukukabiliana na Fumbo la Kifo katika maisha yao. Cheo na madaraka waliyo
nayo yasiwe ni sababu ya wao kushindwa kuingia katika maisha ya uzima wa milele, bali
madaraka yao yawe ni kielelezo cha huduma makini kwa wananchi, daima wakitafuta mafao
ya wengi, ustawi na maendeleo ya wananchi wao.
Viongozi wa Makanisa wanasema,
Marehemu Rais Sata alijielekeza zaidi katika huduma kwa wananchi wa Zambia, akampatia
Mwenyezi Mungu kipaumbele cha kwanza katika maisha na mipango yake. Viongozi wa Kanisa
wanaendelea kusali kwa ajili ya kuombea Zambia wakati huu wa kipindi cha mpito, ili
iweze kuonesha mshikamano wa kitaifa, kukuza na kudumisha amani na utulivu.
Mwili
wa Marehemu Michael Chilufya Sata aliyefariki dunia tarehe 28 Oktoba 2014 Jijini London,
umezikwa kwenye Makaburi ya Viongozi wa Serikali, kwenye Uwanja wa Mabalozi, unaotazamana
na Ofisi za Bunge la Zambia.