2014-11-10 07:55:56

Yapyaisheni maisha ya Familia kwa kusoma Nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican!


Mpendwa msikikizaji wa Kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, tumsifu Yesu Kristo! Kama tulivyokuahidi katika vipindi vilivyopita, karibu tuendelee kushirikiana katika kuyapyaisha mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa II wa Vaticani, ili sote kwa pamoja, kila mmoja kwa nafasi yake na sote kama familia ya Mungu, tuweze kuuishi mtaguso huo maalumu. RealAudioMP3
Kabla hatujasonga mbele, tukumbushane kwa ufupi tu juu ya hati zote za mtaguso huo Mkuu, ili tuone namna zinavyounganika katika kutupatia ujumbe mmoja. Hati hizo zipo katika makundi makubwa matatu. Kuna katiba 4, hizi zimesheheni mafundisho ya kiimani zaidi na hivyo zina hadhi ya ki-nguziimani.
Hati ya kwanza inaitwa Sacrosanctum Concilium. Hati hii inazumgumza juu ya Liturujia Takatifu. Inatuelekeza kuelewa kwa undani zaidi fumbo la sadaka ya Bwana, ukuu wa Mungu na jinsi tunavyopaswa kumwabudu Mungu. Hati ya pili kwa kilatini inaitwa Lumen Gentium, maana yake Mwanga wa Mataifa. Hii inaelezea juu ya fumbo la Kanisa, na inalieleza Kanisa kama Mwanga wa Mataifa. Ya tatu inaitwa Dei Verbum, maana yake Neno la Mungu. Hii inaielezea juu ya Ufunuo wa Kimungu. Hati ya nne inaitwa Gaudium et Spes, maana yake furaha na matumaini. Hii inalielezea Kanisa katika Ulimwengu wa Kisasa.
Kundi la pili la hati za Mtaguso, ni za maagizo mbalimbali. Pamoja na hati za Mafundisho tanzu ya Kanisa, ambazo zinabeba mafundisho-msingi ya Kanisa, Mababa wa Mtaguso walitoa maagizo ya kuyafuata katika nyanja mbalimbali za maisha ya Kanisa. Agizo la kwanza linaitwa Inter Mirifica. Hati hii inaelezea juu ya vyombo vya upashanaji habari. Agizo la pili linaitwa Orientalium Ecclesiarum. Hati hii inahusu Makanisa Katoliki ya Mshariki. Agizo la Tatu linaitwa Unitatis Redintegratio, ambayo inaongelea juu ya Uekumene.
Agizo la nne linaitwa Christus Dominus, hii inaelezea juu ya huduma ya kichungaji ya maaskofu. Agizo la tano linaitwa Perfectae Caritate, inayoongea juu ya kurekebishwa kwa maisha ya wakfu. Agizo la sita linaitwa Optatam Totius. Hii inaongelea juu ya malezi ya Kipadre. Agizo la saba linaitwa Apostolicam Actuositatem, hati ambayo inaongelea juu ya Utume wa walei. Agizo la nane linaitwa Ad Gentes, yaani kwa Mataifa. Ni hati inayoongelea juu ya utendaji wa Kimisionari wa Kanisa. Agizo la tisa linaitwa Presibiterorum Ordinis ambayo inaongelea juu ya huduma na maisha ya Kipadre.
Kundi la tatu la hati za Mtaguso ni Matamko. Nayo yapo matatu tu. Tamko la kwanza ni juu ya malezi ya Kikristo. Mababa walichambua kwa kina sana juu ya suala la malezi katika nyanja zote. Tamko la pili linaitwa Nostra Aetate. Katika hati hii, mababa wanaangazia juu ya Uhusiano wa Kanisa na dini zisizo za Kikristo. Na tamko la tatu linaitwa Dignitatis Humanae, maana yake ni hadhi ya mwanadamu. Ni hati inayozungumzia juu ya Uhuru wa kidini.
Tunazileta hati hizi masikioni mwako mpendwa msikilizaji ili kwa ufupi tu tupate kukumbushwa mababa wa Mtaguso walitaka Kanisa lieleweke, lionekane na litende vipi katika hija yake ya hapa duniani. Kwa kuzidonoa kwa umbali hati hizo zote, leo tuione mmoja tu il ya kwanza ihusuyo Liturujia au utaratibu wa Ibada katika katika Kanisa Katoliki. Hati hii inaitwa Sacrosanctum concilium.
Hati hii ndiyo iliyoleta mageuzi makubwa katika ibada za kanisa katoliki, hasa matumizi ya lugha mahalia za watu, badala ya kutumia kilatini kwa Kanisa zima ambacho si wote walikuwa wanakielewa. Lengo la hati hii ni kutusaidia sisi sote tumwabudu Mungu kama astahilivyo na sisi wenyewe tupate mafaa ya kiroho.
Hati hii pia inasisitiza juu ya malezi ya kiliturujia maseminarini na katika nyumba za kitawa. Kwa njia hiyo waamini wote watasaidiwa kuchota roho halisi ya Kikristo katika chemchemi hiyo ya kwanza na ya lazima; pia wataweza kushiriki ibada kwa ukamilifu wote. Msisitizo wa pekee unapelekwa katika matendo ya kiibada. Ibada zetu zinatuunganisha sote pamoja kama familia ya Mungu, na kwa pamoja tunamwinulia Mungu mioyo yetu, naye kama baba yetu sote anatubariki na kutusikiliza tunapoliitia jina lake kwa pamoja na kwa heshima astahiliyo.
Sura ya pili na ya tatu ya hati hii, inazungumzia juu ya Misa Takatifu, sakramenti na visakramenti, na sura ya nne inazungumzia juu ya sala ya Kanisa. Sura mbili za mwisho zinaelezea kwa kinagaubaga juu ya Muziki na sanaa takatifu. Na inaelekeza kwamba, vipawa mbalimbali vya mwanadamu vitumike katika kumsifu Mungu.
Mpendwa msikilizaji, tunataka mtaguso utue ndani ya familia yako, ndani ya maisha yako. Tunapoitafakari hati hii, wanakanisa la nyumbani tukumbuke wajibu wetu wa kuiishi liturujia. Wakuu wa liturujia takatifu katika familia ni baba na mama. Swali tunalojiuliza sisi wanafamilia ni hili: Mungu mmoja na wa kweli ana nafasi katika familia yetu? Mungu huyo anaabudiwa ipasavyo? Tunasali kwa pamoja kuliitia jina la Mungu ndani ya familia yetu? Vipaji alivyonavyo kila mmoja wetu katika familia yetu, vinamtukuza Mungu na kutuletea usitawi sisi wanafamilia?.
Kisha, sisi kama wanafamilia, tunashiriki vipi katika kuboresha Ibada Takatifu Kanisani? Wanakwaya wanatoka katika familia, wanavyama vya kitume wanatoka katika familia, wahudumu mbalimbali wa misa wanatoka katika familia. Huwa inatokea bahati mbaya ya aibu sana pale ambapo wazazi wanawakataza kabisa watoto wao kushiriki katika mambo ya Kanisa; au wazazi wanakuwa baridi sana katika kuwahimiza watoto wao kwa mambo ya kiroho. Huko ni kulihujumu Kanisa la Nyumbani na Kaniza zima. Sote kwa pamoja tushiriki katika kuboresha Ibada zetu na kulinda unadhifu wake.
Tunarudia tena neno lile, familia ni shule ya sala, ni shule ya liturujia msingi. Ndiko tunafundishwa sala na Ibada na majitoleo kwa watakatifu mbalimbali. Lengo la mabadiliko katika liturujia ya Kanisa ni kujaribu kuwasaidia waamini wasali pamoja, huku wakielewana kwa lugha zao za kawaida. Na sisi katika familia zetu tunaomba na kusihi sana, sala za familia, liturujia ya familia iwe ni chombo cha kuiunganisha familia. Tuwe kitu kimoja, twende pamoja, tutasafiri kwa amani na kufika salama. Lakini kama kila mtu anaabudu alikogeukia, hakika mwovu hataacha kutupepeta kila siku. Tusiyapuuzie mambo ya kiroho na mazoezi yote ya kiroho kwani yana umuhimu mkubwa sana katika kutuunda na kutusindikiza katika maisha yetu ya kila siku. Hadi wakati mwingine tena.

Kutoka katika studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.