Tanzania inahitaji kuwa na mpango miji bora zaidi!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema Tanzania kama nchi inapaswa kuwa na
mpango wa kuendeleza mipango miji (master plan) wa nchi nzima unaozingatia ukuaji
wa miji yetu. Ametoa kauli hiyo Jumatatu, Novemba 10, 2014 wakati akifungua warsha
ya siku tatu ya kuwajengea uwezo Mameya, Wenyeviti na Wakurugenzi wa Halmashauri za
Wilaya na Manispaa za Miji kutoka mikoa yote ya Tanzania Bara. “Sasa hivi hapa
nchini tuna tatizo la ukuaji mkubwa wa miji yetu na Dar es Salaam ni mmojawapo. Hakuna
miundombinu ya majitaka, nyumba zimesongamana, hakuna barabara za uhakika... ukuaji
wa miji ni lazima uangaliwe kwa naman ya tofauti na upewe uzito unaostahili,” alisema. “Lazima
tuje na master plan ya miji yote mikubwa kama Arusha, Mwanza na Dar es Salaam hata
kama itabidi kutafuta wafadhili ili tuweze kuifanya kazi hiyo. Lazima huo mpango kabambe
uwepo kama kweli tunataka kumaliza tatizo hili,” aliongeza. “Hivi hata ukitaka
kupeleka timu ya waokoaji unawapelekaje? Je ukiwapeleka wapite wapi?, watue wapi?
Lazima tutafute wafadhili wa kufinance mpango huu,” alisisitiza. Akitoa mfano Waziri
Mkuu alisema kukosekana kwa mipango miji kunaleta matatizo ya wnanchi kupelekewa mahali
hata kama hapajaandaliwa. “Kulitokea mafuriko hapa Dar es Salaam, watu wakapelekwa
Mabwepande. Je kulikuwa na mpango wowote wa miundombinu ya kuwaweka huko? Je, yakitokea
mafuriko mengine, watu watapalekwa wapi?” alihoji. Alisema kutokuwepo kwa mpango
huo kumefanya asilimia 70 ya makazi kujengwa katika maeneo yasiyo rasmi. Waziri
Mkuu pia aliwataka viongozi hao waangalie ni kwa jinsi gani wanaweza kupunguza athari
zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi kwenye maeneo wanakotoka. “Kwangu mimi natamani
kuona madhara yanayotokana na tabianchi yakipungua. Jaribuni kujiuliza mtaweka mikakati
gani ili kupunguza athari za mafuriko,” alisisitiza. Aliwataka pia waangalie athari
za uchafuzi wa mazingira kwa sababu ni changamoto kubwa katika miji mingi hapa nchini.
“Pale Kinyerezi wana dampo na wanaona suluhisho ni kuchoma moto lakini hawaangalii
madhara ya ule moshi unaotokana na uchomaji taka,” alionya. Mapema, akielezea kuhusu
mkutano huo, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Eng. Mussa Natty alisema mkutano
huo umefanyika ikiwa ni utekelezaji wa makubaliano (Durban Adaption Charter) yaliyofanyika
jijini Durban, Afrika Kusini, Desemba, 2011 ikiwa ni sehemu ya kutafuta ufumbuzi wa
tatizo la mabadiliko ya tabianchi. “Wakati tulipoenda Durban, tulienda na Mkurugenzi
wa Jiji la Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke. Sasa hivi ziko Halmashauri
102 ambazo zimeshatia saini makubaliano haya,”alisema. Lengo la mkutano huo ni
kutafuta njia za kutafuta ufumbuzi wa mabadiliko ya tabia kwa kutumia mbinu zinaoendana
na mazingira ya hapa nchini (local solutions).