2014-11-10 08:19:55

Mitandao ya kijamii ni jukwaa makini la Uinjilishaji


Uwepo wa Kanisa katika mitandao ya kijamii ni jambo la muhimu sana katika mchakato wa majiundo makini ya binadamu katika kukuza mahusiano hasa nyakati hizi za teknolojia ya digitali. Kanisa linapenda kuwasindikiza waamini na watu wote wenye mapenzi mema katika hija yao ya maisha, ili kujenga mahusiano yanayojikita katika mshikamano wa upendo kwa kutambua kwamba, kila mtu ni jirani, kwani ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Huu si mkakati wa shughuli za kichungaji kwa ajili ya Mama Kanisa, bali ni sehemu ya utume na dhamana yake kwa binadamu. Mitandao ya kijamii, ina faida kubwa katika ustawi na maendeleo ya binadamu, lakini pia imekuwa kama dunia ambayo ni tambara bovu! Mahali ambapo kwa sasa kuna changamoto nyingi za kimaadili na utu wema.

Pamoja na mapungufu haya yote, Mama Kanisa anatambua kwamba, mitandao ya kijamii ni Jukwaa makini sana katika kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu, hadi miisho ya dunia. Haya ndiyo yaliyojitokeza kwa uwazi mkubwa wakati wa mkutano wa Wakurugenzi wa Idara za Mawasiliano kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, CCEE, wakati walipokutanika hivi karibuni mjini Athens, Ugiriki, ili kutafakari kwa pamoja kuhusu mawasiliano kama mahali pa kukutana katika ukweli na uhalisia wa maisha.

Mkutano huu umehudhuriwa na Maaskofu 40 pamoja na mabingwa na wataalam wa sayansi ya mawasiliano ya jamii, mkutano ambao ulipata baraka pia kutoka kwa Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii. Wajumbe katika taarifa na shuhuda na majadiliano ya kina, wamekiri kwamba mitandao ya kijamii imeleta mwelekeo mpya katika maisha ya kijamii na kiroho, mambo ambayo yanafanyiwa kazi na Mama Kanisa kwa wakati, ili kutoa majiundo makini yatakayosaidia watu kuwa na matumizi bora na sahihi ya mitandao ya kijamii.

Wajumbe wanakiri kwamba, vijana wa kizazi kipya ndio wanaotumia kwa wingi maendeleo ya teknolojia ya habari, ikilinganishwa na watu wenye umri mkubwa ambao wengi wao wamebaki kidogo nyuma, changamoto kwa Mama Kanisa kutumia fursa hii, ili vijana waweze kuwa na mahusiano thabiti si tu katika maisha yanayoelea katika ombwe, bali kwa kujikita katika uhalisia wa maisha!

Mitandao ya kijamii ni jukwaa la maisha na wala si tu kitendea kazi, kumbe kuna haja ya kukazia kile kinachowekwa kwenye mtandao kiwe ni uhusiano na maisha ya watu kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko. Lengo ni kusaidia ili kweli, watu waguswe katika undani wa maisha yao: kiakili, kiroho na kimwili, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo amewaletea ukombozi na maisha mapya kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake.
Kanisa halina budi kuhakikisha kwamba, ujumbe wake unawagusa watumiaji wa mitandao ya kijamii. Kanisa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, linaendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali ambazo halina budi kuzifanyia kazi, ili kuhakikisha kwamba, kweli Injili ya Furaha inawafikia Watu wa Mataifa.

Mitandao inayomilikiwa na kusimamiwa na Kanisa imeendelea kuwa na mvuto kwa watu wengi wanaotaka kuzima kiu yao kuhusu kweli za Kiinjili. Uwanja wa mawasiliano ya kijamii una kero na kinzani zake kwa Kanisa na Mafundisho yake, lakini bado Mama Kanisa anataka kuhakikisha kwamba, “anakula sahani moja” na watumiaji wa mitandoa ya kijamii hadi kieleweke!

Makanisa mahalia yanachangamotishwa kuhakikisha kwamba, yanajihusisha katika matumizi ya njia za mawasiliano ya kijamii, ili kutangaza maisha na utume wa Kanisa kwa watu mahalia. Kwa Makanisa yale ambayo waamini wake wengi ni watumiaji wazuri wa mitandao ya kijamii, wanaweza kushirikishana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa mahalia, kwa kujenga mahusiano ya karibu zaidi.

Katika ulimwengu wa mawasiliano ya kijamii, Mama Kanisa anataka kudumisha: umoja na mshikamano kati ya watu, ili kukoleza maboresho ya mahusiano na maisha ya kijamii yanayojikita katika matumizi ya mitandao ya kijamii.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.