2014-11-10 08:03:14

Mchakato kuelekea umoja wa kitaifa!


Burkina Faso imefungua ukurasa mpya kwa Serikali ya kijeshi inayoongozwa na Luteni Kanali Isaac Zida kwa kuanza na mchakato wa upatanisho wa kitaifa ili hatimaye, kurejesha utawala wa kiraia nchini humo ifikapo mwezi Novemba 2015. Serikali ya kijeshi imetoa pia fursa kwa viongozi wa Chama cha CDP kilichokuwa kinaongozwa na Rais Blaise Compaorè aliyebwaga manyanga hivi karibuni, kushiriki katika mchakato wa kuunda Serikali ya mpito.

Vyama vya kisiasa na kijamii nchini Burkina Faso vimeridhia vigezo na sifa anazopaswa kuwa nazo mwananchi wa Burkina Faso atakepewa dhamana ya kuongoza Serikali ya kipindi cha mpito hadi kufikia uchaguzi mkuu, hapo mwakani.

Luteni Kanali Issac Zida ametupilia mbali vitisho vilivyotolewa na Umoja wa Afrika kwa kuitaka Serikali ya kijeshi kuhakikisha kwamba, inarudisha madaraka mikononi mwa raia katika kipindi cha siku kumi na tano, vinginevyo, ingekiona kile kilichomnyoa Kanga manyoya! Luteni Kanali Zida anasema, jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, Burkina Faso inafikia muafaka wa kitaifa, ili hatimaye, kuweza kufanikisha mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Novemba 2015 kwa kuzingatia misingi ya haki, amani na utulivu.








All the contents on this site are copyrighted ©.