Sakata la magendo ya pembe za ndovu kati ya China na Tanzania!
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa nchini Tanzania Bwana BERNAD MEMBE
ameutaarifu umma wa watanzania na dunia kwa ujumla kwamba madai yaliyotolewa na taasisi
isiyo ya kiserikali ya London Environmental investigation Agency EIA hayana ukweli
wowote.
Pia amekanusha madai ya kwamba serikali ya Tanzania haijali na wala
haichukui hatua dhidi ya wanaojishughulisha na biashara haramu ya pembe za ndovu.
Akitoa tamko la serikali kuhusiana na shutuma iliyotolewa na taasisi hiyo dhidi ya
serikali ya Tanzania Bungeni mjini Dodoma, MEMBE amesema taarifa hizo zote ni za
kupikwa na kuungwa mkono ili kuchafua heshima ya Tanzania na heshima ya Taifa la China.
Ametaja
sababu za kusema taarifa hizo ni za uongo kuwa taarifa kama hiyo sio mara ya kwanza
kutolewa iliwahi kutolewa mwaka 2013 na mtoa taarifa ambaye ametajwa kuwa chanzo cha
habari ni mtu mmoja ambaye walimkuta barabarani na kuanza kumuuliza maswali hali sio
mtumishi wa bandari wala uwanja wa ndege.
Mbali na hilo amesema ziara ya rais
huyo wa China ilikuwa ya masaa 24 na programu yake ilianza mara tu alipowasili nchini
kuanzia saa 9 alasiri hadi saa 4 usiku kwenye dhifa ya Taifa na kuhoji hizo shopping
zinazoelezwa kufanywa na ujumbe wa rais huyo zilifanywa muda gani.
Mheshimiwa
MEMBE amewataka watanzania kutokubali upuuzi wa aina hiyo kwa kuwa Tanzania ni Taifa
huru halichaguliwi marafiki wala halirithishwi maadui na kuahidi kuendeleza ushirikiano
uliopo wa kidugu na China na kwame hawarudi nyuma kutokana na maneno ya uwongo na
uzushi.
Vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi vilitoa habari kwamba ujumbe
wa rais wa China uliokuja nchini Tanzania miezi 18 iliyopita ulijihusisha na ununuzi
wa pembe za ndovu nchini Tanzania na chanzo cha habari kikiwa ni kutoka kwa Taasisi
hiyo ya EIA.
Wakati huo huo Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
wameridhia azimio la kumpongeza spika wa bunge hilo mheshimiwa ANNE MAKINDA kwa kuchaguliwa
kuwa rais wa Jukwaa la Mabunge ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa
Afrika (SADC-PF).
Akisoma azimio hilo bungeni mjini Dodoma Mwenyekiti wa kamati
ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa mheshimiwa MUSSA ZUNGU amemzungumzia mheshimiwa
MAKINDA kuwa ni mzoefu wa kutosha katika medani za siasa na uongozi kwa zaidi ya miaka
37 kwa kushika nyadhifa mbalimbali kitaifa na kimataifa.
Amesema kutokana na
jitihada mbalimbali zinazofanywa na rais JAKAYA KIKWETE za kuitangaza nchi ya Tanzania
zilisaidia sana katika mchakato wa kumnadi mheshimiwa MAKINDA kwa wajumbe wa mkutano
na kufanikiwa kushinda kwa kishindo bila ya kupingwa.
Wakiunga mkono azimio
hilo baadhi ya wabunge waliochangia wamempongeza mheshimiwa MAKINDA na kusema ni mtu
anayestahili kupata nafasi hiyo kutokana na uchapakazi wake.
Mbunge wa Kigoma
Kaskazini mheshimiwa ZITTO KABWE amesema kwa mara nyingine tena Tanzania imeshamiri
katika medani ya dunia kitu ambacho kinaleta heshima kubwa na ni ishara ya mafanikio
makubwa ya kidiplomasia katika nyanja ya kimataifa.
Amesema kupata kwake nafasi
hiyo kunaonyesha wazi kuwa ni jinsi gani bunge la Jamhuri lilivyokuwa halikufanya
makosa kumchagua kuwa spika na kusema ana aamini atapeperusha bendera ya Tanzania
vizuri anakokwenda na kuwataka wabunge kumuunga mkono kwa kuwa ni mtu mzuri.
Kwa
upande wake mbunge wa viti maalum mheshimiwa BERNADETA MUSHASHU ameungana na wengine
kumpongeza na kusema hawakukosea kumchagua kwa kuwa sifa anazo kutokana na kuandaliwa
na Taifa hili na kumuomba mungu ampe uwezo mkubwa wa kupeperusha bendera ya Tanzania.
Mbunge
wa viti maalum mheshimiwa RUKIA AHMED amesema anaona fahari kutokana na ushindi huo
na kwamba uteuzi huu haujaja bure bali umekuja kutokana na juhudi kubwa alizonazo
katika utendaji kazi wake wa kutobagua dini,kabila wala vyama vya siasa.
Wakati
huo huo mheshimiwa MAKINDA amewataka wabunge wa vyama vyote vya siasa kuamka na kubadilisha
fikra zao ili wafikirie Maendeleo.
Mheshimiwa MAKINDA akitoa shukrani kwa wabunge
amesema Maendeleo sio Taifa bali yanapaswa kuanzia kwa wabunge wenyewe kwa kuwa hivi
sasa nchi nyingi duniani wanachosimamia ni suala la uchumi na upo uwezekano wa Tanzania
kama wasiposimamia msingi huo ikabaki nyuma.
Amewataka kuamka na kusimamia
suala hilo ingawa mwaka huu ni mgumu kwa sababu wanaelekea kwenye uchaguzi lakini
isiwe sababu ya kuacha kufanya kazi na kuanza kupigana vijembe.