2014-11-07 10:53:46

Wakristo na Wasikhi wanahamaishwa kudumisha huduma ya upendo!


Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini limewaandikia waamini wa dini ya Kisikh ujumbe wa amani, matashi mema na mshikamano wa kidugu katika maadhimisho ya Siku kuu ya Guru Nanak Jayanti, iliyoadhimiwa, hapo tarehe 6 Novemba 2014 kwa kuongozwa na kauli mbiu "Wakristo na Wasikhi: kwa pamoja dumisheni huduma ya upendo".

Sherehe hizi zisaidie kujenga na kudumisha mshikamano, utulivu na amani, wakati wanapotoa huduma katika Jamii. Kwa Wakristo, Yesu Kristo ni kielelezo cha matendo ya huruma kama inavyojionesha katika Maandiko Mtakatifu, kwa kujifananisha na Msamaria mwema. Kwa Wasikhi, upendo na huduma ni mambo yanayopewa kipaumbele cha kwanza katika maisha yao, kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, wagonjwa, wazee, wahamiaji, wakimbizi, wanaodhulumiwa na kunyanyaswa, kwa kutambua kwamba, binadamu wote ni kazi ya Mwenyezi Mungu.

Upendo na majitoleo binafsi katika huduma ni mambo muhimu sana katika kukuza upendo na mshikamano na wengine. Kila mtu anapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa utu na heshima yake kwani ana thamani ya pekee mbele ya Mwenyezi Mungu kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.