Shikamaneni kidugu katika Kristo ili kukabiliana na changamoto mamboleo!
Fumbo la Ekaristi Takatifu ni kielelezo cha umoja na mshikamano kati ya watu wa Mungu
na matunda yake ni kupenda kusoma na kulitafakari Neno la Mungu, ili kuishi kadiri
ya matakwa ya Injili pamoja na kuendeleza upendo, urafiki, udugu na mshikamano kati
ya watu, tayari kusoma alama za nyakati, huku waamini wakimsikiliza Roho Mtakatifu
kwa unyenyekevu.
Huu ndio ushuhuda unaojikita katika udugu unaofumbatwa katika
maisha ya Kikristo, alama wazi yenye mvuto na mguso katika imani kwa Kristo Mfufuka.
Ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 7 Novemba
2014 alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa Chama cha Fokolare, waliomtembelea mjini
Vatican kwa kukazia kwamba, Wakristo wanapaswa kuungana na kutekeleza changamoto mbali
mbali zinazojitokeza katika uso wa dunia kwa njia ya mshikamano wa kidugu.
Kwa
njia hii wataonesha kwa imani katika matendo utandawazi wa mshikamano na udugu miongoni
mwa Wakristo. Katika nchi nyingi bado kunakosekana uhuru wa kuabudu na kuishi kiaminifu
kadiri ya kanuni maadili ya Kikristo; kuna Wakristo wanaoendelea kunyanyaswa na kudhulumiwa
kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake; vitendo vya kigaidi vinazidi kushika
kasi ya ajabu; bado kuna mateso na mahangaiko kwa wakimbizi na wahamiaji; misimamo
mikali ya kiimani; tatizo la watu kukumbatia malimwengu; mambo ambayo yanapaswa kupewa
uzito wa pekee katika dhamiri kama Wakristo na Viongozi wa Kanisa.
Katika changamoto
za namna hii anasema Baba Mtakatifu, kuna haja ya kutafuta njia mpya na endelevu zinazosimikwa
katika uvumilivu, ili kufikia umoja na hatimaye, kuwawezesha watu kuamini, kwa kuonesha
imani na ujasiri unaofumbatwa katika maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, kielelezo
cha umoja na mshikamano.
Mtakatifu Paulo anaonesha kwa namna ya pekee kwamba,
Ekaristi Takatifu ni kiini cha maisha ya Kikristo, wakati wa ukweli na fursa ya kukutana
na neema kutoka kwa Yesu kwa njia ya uwajibikaji. Kwa njia ya Fumbo la Ekaristi, waamini
wanatambua kwamba, umoja ni zawadi inayowawajibisha. Baba Mtakatifu Francisko amewatakia
wajumbe wa Chama cha Kitume cha Wafokolari kuzaa matunda ya ukomavu katika kudumisha
umoja, huku wakishuhudia udugu.