2014-11-06 08:15:17

Mwongozo na sera mpya ya fedha kwa ajili ya taasisi na ofisi za Vatican


Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Uchumi mjini Vatican anasema, Sektretarieti yake imechapisha mwongozo na sera ya fedha kwa taasisi na ofisi mbali mbali zinazoendeshwa na Vatican na kwamba, mwongozo huu utaanza kutumika tarehe Mosi, Januari 2015. Mwongozo umepitishwa tayari na Baba Mtakatifu Francisko pamoja na Baraza la Kipapa la Uchumi.

Lengo la Mwongozo huu anasema Kardinali Pell ni kuzisaidia taasisi na ofisi mbali mbali za Vatican kufanya maboresho makubwa katika vigezo na mchakato wa utekelezaji wa Bajeti kwa kuwa na kanuni za pamoja zinazozingatia viwango cya kimataifa. Mkazo ni kuhakikisha kwamba, rasilimali fedha, watu na mali ya Kanisa vinatumika kikamilifu kwa ajili ya huduma na utume wa Mama Kanisa Ulimwenguni.

Mwongozo na Sera ya Fedha zitaendelea kuimarisha mchakato wa mabadiliko makubwa yanayofanywa na Kanisa kwa wakati huu ili kuongeza tija, ubora, ufanisi, ukweli na uwazi katika matumizi ya mali ya Kanisa. Hatima ya mwongozo huu anasema Kardinali Pell ni kuiwezesha Vatican kutekeleza sera mpya katika masuala ya fedha na rasilimali ya Kanisa, kwa kuwa na mwelekeo mpana zaidi.

Haya ni mabadiliko ambayo Makardinali walishauri yafanyiwe kazi wakati wa mikutano yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Matumizi ya fedha ya Kanisa yatakaguliwa na kuhakikiwa na taasisi ya kimataifa, ili kudumisha dhana ya ukweli na uwazi katika matumizi ya mali ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.