2014-11-06 09:56:10

Mshikamano wa Baraza la Makanisa kwa wananchi wa Nigeria!


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni amesikitishwa na mashambulizi yanayofanywa na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haramu dhidi ya Makanisa nchini Nigeria. Baraza la Makanisa Ulimwenguni linapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati kwa wananchi wote wa NIgeria walioguswa kwa namna ya pekee na mashambulizi ya kigaidi ambayo yamekuwa ni tishio kwa maisha na usalama wa watu na mali zao.

Baraza la Makanisa linawapongeza wale wote wanaojitahidi kuwahudumia watu walioathirika kutokana na mashambulizi kwa kuyakimbia makazi yao ili kutafuta usalama wa maisha, hasa Kaskazini mwa Nigeria. Hadi sasa wasichana 200 waliotekwa nyara hawajulikani mahali walipo na inasemekana kwamba, wamekwisha wekwa unyumba na watesi wao, jambo ambalo halikubaliki kamwe anasema Dr. Tveit.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linaiomba Serikali ya Nigeria kuendelea kushughulikia tatizo la wasichana hao ili waweze kuachiliwa huru haraka iwezekanavyo. Ni wazi kwamba, Nigeria inahitaji msaada kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa ili kupambana na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram, kwani hatima na Nigeria iko mashakani, watu wanaendelea kuteseka na kukata tamaa.

Baraza la Makanisa linawaalika watu wote wenye mapenzi mema kuwasindikiza wananchi wa Nigeria kwa sala zao katika kipindi hiki kigumu!







All the contents on this site are copyrighted ©.