Jielekezeni zaidi katika ustawi na maendeleo ya Familia nchini Malawi!
Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 6 Novemba 2014 amewapongeza na kuwashukuru
Maaskofu Katoliki kutoka Malawi wanaofanya hija ya kitume mjini Vatican, kwa sadaka
na majitoleo yao kwa ajili ya kuwahudumia Watu wa Mungu nchini Malawi, kwa kujikita
katika umoja; haki, amani na upatanisho; mambo msingi yanayoongoza mchakato wa Uinjilishaji
wa kina, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Malawi kwa ujumla.
Licha ya changamoto
nyingi ambazo wananchi wa Malawi wanakabiliana nazo katika medani mbali mbali za maisha,
lakini bado familia inapewa kipaumbele cha kwanza katika kuwafunda vijana katika maadili
na utu wema; kwa kukazia upendo wa dhati, sadaka, uaminifu pamoja na kuendeleza mchakato
wa Malawi katika ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika mshikamano wa dhati.
Familia
inakabiliwa na changamoto mbali mbali kwa nyakati hizi, Maaskofu kama Mababa na wachungaji
wanaalikwa kulea, kulinda na kuimarisha familia mintarafu tunu msingi za kiimani,
ili kuimarisha maisha na utume wa Kanisa ndani ya Familia. Baba Mtakatifu anawataka
Maaskofu wa Malawi kuona ukweli kuhusu maisha ya ndoa na familia katika harakati za
kutangaza Injili, ili familia nzima na makando kando yake ipate kuponywa na kuimarishwa
na upendo unaobubujika kutoka katika Injili na kufundishwa na Mama Kanisa.
Baba
Mtakatifu Francisko analitaka Kanisa nchini Malawi kujielekeza zaidi katika shughuli
zake za kichungaji kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya familia, kwa kuponya na kuimarisha
tunu msingi za maisha ya kifamilia; kwa kufundisha na kuinjilisha familia, hasa zile
zinazokabiliana na matatizo, kinzani na changamoto mbali mbali, ili Kanisa liweze
kustawi na Malawi kupata maendeleo zaidi.
Kwa kuwa na familia imara, Kanisa
linaweza kupata Mapadre na Watawa ambao wako tayari kujisadaka kwa ajili ya huduma
kwa jirani zao pamoja na kuendelea kuimarisha ari na moyo wa shughuli za kimisionari,
ili kuwajengea waamini wa Malawi uwezo wa kuinjilisha, ili hatimaye, kushirikisha
utajiri huu kwa Kanisa zima, daima kwa kutafuta mema kwa ajili ya wengine, sanjari
na kuimarisha upendo kwa Makanisa ambayo yana upungufu mkubwa wa wahudumu wa Injili.
Baba
Mtakatifu anawataka Maaskofu kuwa karibu na Mapadre wao, kwa kuwasikiliza na kuwahudumia
kwa upendo wa kibaba unaojikita katika sadaka binafsi. Mapadre watambue na kuonja
upendo kutoka kwa Maaskofu wao, daima wakijitahidi kuwapatia majiundo makini yanayogusa
mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili; Waseminari na Watawa waandaliwe barabara
ili kuweza kutekeleza majukumu na dhamana yao kwa ufanisi mkubwa, ili waweze kujisadaka
kwa furaha, kama kielelezo cha ukomavu wa majiundo yao katika azma ya Uinjilishaji
mpya kwa Malawi na Ulimwengu katika ujumla wake.
Baba Mtakatifu anawahimiza
Maaskofu wa Malawi kuendelea kuwafunda vijana wa Malawi, kwa kuwapatia ukweli wa imani
na furaha inayobubujika katika utekelezaji wa kanuni maadili. Vijana wahubiriwe kwa
ari na moyo mkuu unaobubujika upendo kwa Kristo na Kanisa lake; kwa kuimarisha misingi
ya familia bora ili kujenga haki na fadhila mbali mbali.
Baba Mtakatifu anawakumbuka
kwa namna ya pekee wananchi wa Malawi wanaoogelea katika dimbwi la umaskini na wagonjwa
wa Ukimwi, kwa kulitaka Kanisa kuendelea kuonesha mshikamano na upendo na wananchi
hao, kwa njia ya mikakati ya kichungaji, sala na huduma makini, kwa kutambua kwamba,
Kristo alikuja hapa duniani ili kuganga na kuwaponya watu, ili waweze kupata maisha
mapya. Baba Mtakatifu anawapongeza Maaskofu kwa kuwa karibu na wagonjwa pamoja na
maskini nchini Malawi.