2014-11-05 09:55:26

Ubinafsi ni sumu inayotishia ustawi na maendeleo ya familia


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwenda kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa wanaoendelea na mkutano wao wa mwaka uliofunguliwa Jumanne tarehe 4 Novemba 2014 amewataka Maaskofu kuendelea kuwatangazia Watu wa Mungu Injili ya Furaha; kwa kukuza na kudumisha moyo na ari ya kimissionari.

Baba Mtakatifu anaitakia Familia ya Mungu nchini Ufaransa maandalizi mema kwa ajili ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani utakaozinduliwa Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, yaani tarehe 30 Novemba 2014. Ni mwaka maalum wa faraja na matumaini kwa Familia ya Mungu.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko anawapongeza Maaskofu Katoliki kutoka Ufaransa kwa kuchagua mada ambazo zinashuhudia utashi wa Maaskofu Katoliki Ufaransa wa kujenga Kanisa ambalo malango yake yako wazi pamoja na kuwataka kuendelea kuonesha mshikamano wa upendo na udugu na Wakristo wanaoishi huko Mashariki ya Kati.

Wakati huo huo, Askofu Georges Pontier, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa, katika hotuba yake ya ufunguzi amekazia umuhimu wa familia kama chombo kinachohifadhi maisha, ambayo kwa sasa yako hatarini kutokana na sheria zinazokumbatia utamaduni wa kifo, kwa kushinikiza ndoa za watu wa jinsia moja pamoja na kuendekeza kifo laini. Ubinafsi, usawa wa kijinsia na haki binafsi ni kati ya mambo yanayohataraisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia nchini Ufaransa.

Baraza la Maaskofu katika mkutano wake utakaohitimishwa hapo tarehe 9 Novemba 2014 wamgusia pia masuala ya kimataifa kama vile kinzani na migogoro ya kivita inayoendelea huko Ucrain, Mashariki ya Kati, nyanyaso na dhuluma za kidini sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.