2014-11-05 14:35:36

Onesheni haki, huruma na ukarimu wa Mama Kanisa kwa wote wanaomkimbilia katika shida na mahangaiko yao ya ndani!


Baba Mtakatifu Francisko kabla ya kutoa Katekesi yake, Jumatano asubuhi tarehe 5 Novemba 2014 amekutana na kuzungumza na wajumbe wanaoshiriki katika kozi maalum juu shughuli zinazofanywa na Mahakama kuu ya Rufaa ya Vatican, kwa kuwataka wahusika kuhakikisha kwamba, wanatenda haki kwa kuharakisha kutoa maamuzi ya kesi mbali mbali ambazo wanazofanyia kazi.

Baba Mtakatifu anasema, ameunda Tume maaluma itakayoandaa kanuni msingi katika masuala ya haki na upendo, ili kuwasaidia watu kupata maamuzi ya Kanisa kuhusiana na masuala ya ndoa yanayofikishwa Mahakani hapo, kwa kuzingatia haki! Kesi za ndoa zinazokatiwa rufaa zinachukua muda mrefu kiasi cha kuwakatisha watu tamaa pamoja na ukweli kwamba, Mahakama hizi ziko mbali sana na maisha ya watu wa kawaida, hali inayogumisha upatikanaji wa haki katika masuala ya ndoa. Mahakama kuu ya Rufaa inapaswa kutoa maamuzi ya haki, ili kuwaweka watu huru na vifungo vya ndoa.

Baba Mtakatifu amewataka wafanyakazi wa Mahakama kuu ya Rufaa kuwa makini zaidi ili wasimezwe na malimwengu wakajikuta wanatumbukia katika rushwa, mambo yanayosababisha kashfa ndani ya Kanisa. Wafanyakazi waoneshe ukarimu, haki na huruma ya Mama Kanisa kwa wale wanaomkimbilia katika shida na mahangaiko yao ya ndani; wamepewa bure na wao wanapaswa kutoa bure, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya roho za waamini.







All the contents on this site are copyrighted ©.