2014-11-05 07:48:18

Familia ni chemchemi ya maisha!


Askofu mkuu Josè Manuel Imbamba, msemaji mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Angola, Sao Tome na Principè, katika mahojiano maalum na Radio ya Taifa nchini Angola anabainisha kwamba, Kanisa Katoliki litaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu na kukataa kishawishi cha kutaka kuiga mambo ya kigeni na hatimaye, kumezwa na malimwengu.

Askofu mkuu Imbamba anasema, kuna mambo ambayo ni kinyume cha maadili na utu wema, lakini kwa baadhi ya Jamii yameanza kuonekana kuwa ni mambo ya kawaida na wala hakuna tena soni kuona watu wa jinsia moja wakiishi kwa pamoja kama bwana na bibi; mambo ambayo baadhi ya Jamii wanataka kuyahalisha kwa kuyapigia debe, ili yakubalike! Hii si haki wala busara!

Upendo kati ya Bwana na Bibi hauna budi kulindwa na kudumishwa kwani hapa ni mahali patakatifu ambapo uhai wa mwanadamu unapata chimbuko lake, tayari kushiriki katika kazi ya uumbaji, ambayo Mwenyezi Mungu amemdhamisha mwanadamu. Familia kadiri ya mpango wa Mungu haina budi kukuzwa na kudumishwa, kwa kuwasaidia na kuwasindikiza wanandoa watarajiwa na wanandoa wapya katika hija ya maisha yao, wanapojitahidi kujenga familia kama Kanisa dogo la nyumbani.

Wanandoa wapate msaada kutoka ndani ya Kanisa, ili kuimarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia zinazojikita katika upendo usiogawanyika, udumifu, uaminifu, majadiliano, heshima; huruma na msamaha pamoja na ukuaji wa mtu mzima: kiroho na kimwili.







All the contents on this site are copyrighted ©.