2014-11-04 07:56:05

Suala ya wahamiaji na wakimbizi Barani Ulaya ni tete na nyeti!


Padre Tumaini Litereku, kutoka Jimbo kuu la Songea, Tanzania ambaye kwa sasa anasoma nchini Ujerumani katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, suala la wakimbizi na wahamiaji kutoka Barani Afrika wanaotafuta hifadhi na ubora wa maisha ni tete na nyeti, linahitaji kuangaliwa kwa mapana zaidi, kwani mambo yanazidi kubadilika kila kukicha! RealAudioMP3

Kuna baadhi ya watu wanadhani kwamba wakishapata fursa ya kutia mguu Barani Ulaya, mambo yao yatakuwa yamewanyookea na hapo umaskini wataupatia kisogo na kuanza kupeta kwa kula kuku kwa mrija! Lakini, ukweli na uzoefu wa mambo unaonesha kwamba, licha ya mafanikio makubwa yanayoonekana Barani Ulaya na kwingineko ni matokeo ya mchakato mkubwa katika maisha ya watu. Watu wasidhani kwamba, kwa kuzamia meli au kwa kutafuta njia za mkato ili kufika Ulaya ni tiketi ya mafanikio. Kuna watu wanateseka na utu wao kudhalilishwa kutokana na ndoto kama hizi.

Padre Litereku anasema, pale inapowezekana watu wajitahidi kutafuta na kuboresha maisha yao kwa juhudi na maarifa wakiwa ndani ya nchi zao wenyewe, kwani hii ni haki yao msingi. Ni wajibu wa Serikali husika kuhakikisha kwamba, zinaweka mazingira mazuri kwa wananchi wao ili waweze kufaidika kwa fursa mbali mbali zinazopatikana ili kujiletea maendeleo endelevu. Ili kufikia lengo hili, wahenga waliwahi kusema kunahitajika: siasa safi, uongozi bora na ardhi.

Zama za kuzamia meli kwa ajili ya kutafuta maisha bora Barani Ulaya kwa sasa zimepitwa na wakati, kwani huu ni mwanzo wa kuweka maisha rehani, kwani si mchezo watu wanazama na kufa maji baharini; watu wanadhulumiwa na kunyanyaswa na pale wachache wanapofaulu kufika Ulaya wanajikuta wamefungiwa kwenye kambi za wakimbizi na wahamiaji na hapo ndiyo mwisho wa ndoto ya kula kuku kwa mrija wakiwa Ulaya, kwani hali inakuwa ni mbaya zaidi kuliko hata pengine walivyoiacha katika nchi zao za asili.

Padre Tumaini Litereku, watu wajitahidi kubaki na kutafuta riziki na maisha bora zaidi katika nchi zao wenyewe. Kwa wale wanaotaka kutafuta riziki ya kijani kibichi Ulaya, basi watumie njia halali na kwa kuzingatia sheria, vinginevyo watajikuta wakidhalilishwa na hatimaye kupoteza matumaini ya maisha!







All the contents on this site are copyrighted ©.