2014-11-03 09:17:32

Utunzaji bora wa mazingira ni suala linalogusa haki na kanuni maadili


Mapambano dhidi ya baa la umaskini pamoja na utunzaji bora wa mazingira ni kati ya mambo msingi yanayopaswa kufanyiwa kazi na Jumuiya ya Kimataifa mara baada ya kuhitimisha utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015. Dunia inakabiliwa na madhara makubwa yanayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, mambo yanayochangiwa kwa kiasi kikubwa na ulaji wa kupindukia pamoja na uzalishaji mkubwa wa hewa ya ukaa kutoka katika viwanda.

Askofu mkuu Bernadito Auza, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa anasema kwamba, ujumbe wa Vatican unaliangalia suala hili si tu katika miwani ya mazingira bali ni suala linalogusa haki na kanuni maadili, kwa kuwasaidia maskini wanaoathirika zaidi kutokana na madhara ya mabadiliko ya tabianchi sanjari na kuwajengea uwezo wa kuwa na teknolojia rafiki, itakatoweza kudhibiti uchafuzi wa mazingira.

Jumuiya ya Kimataifa inaanza kuelekeza macho yake kwenye mikutano mikubwa ya kimataifa itakayofanyika hapo mwakani 2015, ambako Jumuiya ya Kimataifa inatarajiwa kupata muafaka wa makubaliano juu ya udhibiti wa uzalishaji wa hewa ya ukaa, kwa kutambua kwamba, kila mtu anawajibika kwa kiasi chake, kulinda na kutunza mazingira. Hii inatokana na ukweli kwamba, ulimwengu kwa sasa unaonekana kama kijiji na hivyo unahitaji uwajibikaji wa pamoja, kwa ajili ya usalama na ustawi wa watu kwa sasa na kwa siku zijazo.

Changamoto ya utunzaji bora wa mazingira inahitaji siasa safi na mikakati makini ya kiuchumi, itakayotekelezwa na Jumuiya ya Kimataifa, kwa kuzingatia ukweli wa tafiti za kisayansi; kwa kuelewa na kutekeleza mikakati itakayopangwa kama sehemu ya agano la kimaadili ili kutunza mazingira. Kila mtu anapaswa kutekeleza wajibu wake kadiri ya uwezo na fursa alizo nazo, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.