2014-11-03 07:21:19

Baada ya kifo kuna maisha ya uzima wa milele!


Kifo si kigingi cha maisha ya binadamu, kwani binadamu ameumbwa na Mwenyezi Mungu ili aweze kufurahia maisha yenye uzima wa milele. Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 2 Novemba 2014 wakati Mama Kanisa alipokuwa anaadhimisha Siku ya Marehemu wote.

Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea marehemu wote waliofariki dunia wakati wa vita, kinzani; kwa wakristo waliouwawa kikatili kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake bila hata ya kubahatika kupata Sakramenti za Kanisa au hawakuweza kupata muda wa kusali na kutubu. Amewakumbuka hata wale ambao hawana mwombezi, watu ambao wamesahaulika kabisa; watu ambao wamefariki dunia kutokana na baa la njaa na umaskini; watu wambao wamejisadaka kwa ajili ya kutoa huduma kwa jirani zao.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu amewakumbuka wale wote waliofariki dunia katika kipindi cha mwaka huu, huku wakiwa na imani na matumaini kwa Yesu Kristo aliyemwaga Damu yake Azizi kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Baba Mtakatifu katika sala yake, anamwomba Mwenyezi Mungu kutoangalia umaskini, magonjwa na masumbuko ya binadamu, wakati watakapokuwa wanajongea mbele ya uso wake kwa ajili ya hukumu kwa wenye haki kufurahia maisha ya uzima wa milele na wadhambi kuingia motoni.

Baba Mtakatifu anamwomba Mwenyezi Mungu aoneshe uso wenye huruma unaomsindikiza mwanadamu katika hija ya maisha yake, ili aweze kujitakasa na hatimaye, kupokelewa kwenye huruma ya Mungu isiyokuwa na mwisho. Anamwomba awaokoe watoto wake wasije wakapotelea kwenye moto wa milele, mahali ambapo hakuna tena fursa ya kutubu.

Baba Mtakatifu ameziweka roho za waamini marehemu hasa wale ambao wamefariki dunia bila kupata Sakramenti za Kanisa au kutubu na kumwongokea Mungu wakati walipokuwa wanakunja maisha yao hapa duniani, mikononi mwa huruma ya Mungu. Amemwomba Mwenyezi Mungu awajalie watoto wake neema, ili kifo kitakapowadia kiwakute wanakesha, ili hatimaye, waweze kupata pumziko la milele huko mbinguni.

Baba Mtakatifu anasema, Siku ya kuwakumbuka Marehemu wote ina uhusiano wa pekee na Siku kuu ya Watakatifu wote; kama ilivyo furaha na majonzi yaliyojionesha wakati wa maisha ya Yesu Kristo, muhtasari wa imani na matumaini ya Kikristo. Mama Kanisa anaposafiri hapa dunia anafurahia maombezi ya Watakatifu na Wenyeheri, wanaosaidia kuenzi utume wa Kanisa katika utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu. Kwa upande mwingine, anashiriki pia kilio cha watoto wake wanaofariki dunia na hivyo kumshukuru Mungu kwa kuwakomboa kutoka katika lindi la dhambi na mauti.

Baba Mtakatifu amewakumbuka wale wote wanaotumia muda wao kwa ajili ya kutembelea Makaburini, mahali ambapo waamini wamelala usingizi wa amani na wataweza kuamshwa na Yesu Kristo mwenyewe. Kifo cha mwili wa mwanadamu ni kama usingizi, ndiyo maana Mama Kanisa anawahimiza watoto wake kusali kwa ajili ya kuwaombea marehemu, lakini kwa namna ya pekee kabisa kwa njia ya maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, msaada wa pekee ambao unaweza kutolewa na waamini hapa duniani kwa ajili ya roho za marehemu hasa wale waliosahaulika kama wanavyohimiza Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kwa kuonesha umoja katika Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa.

Baba Mtakatifu anawahimiza waamini kutunza makaburi na kuwaombea marehemu, kama kielelezo cha imani na matumaini kwa kutambua kwamba, kifo si hatima ya maisha ya mwanadamu, kwani mwanadamu ameumbwa ili kupata maisha ya uzima wa milele yanayopata chimbuko lake kwa Mungu mwenyewe.

Waamini wanahimizwa kumwomba Bikira Maria aliyeonja mateso ya Mwanaye Yesu Kristo pale chini ya Msalaba, lakini baadaye akashiriki katika furaha ya Ufufuko wa Mwanaye mpendwa na kwamba, daima yuko karibu na wote wanaomkimbilia kwa imani na matumaini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.