2014-10-30 09:18:18

Sri Lanka inamsubiri Papa Francisko kwa mikono miwili!


Kardinali Malcolm Ranjith, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Colombo nchini Sri Lanka, wakati akizungumza na Mapadre wa Jimbo lake amethibitisha kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anatazamiwa kutembelea Sri Lanka kuanza tarehe 13 hadi tarehe 15 Januari 2015.

Mapadre wametakiwa kuwajulisha waamini pamoja na taasisi zinazosimamiwa na kuongozwa na Kanisa Katoliki, ili kuanza maandalizi ya kina kwa ajili ya ujio wa Baba Mtakatifu Francisko nchini mwao. Waamini kwa namna ya pekee, wanahimizwa kusali, ili hija hii ya kichungaji iweze kufanikiwa na kuzaa matunda yanayokusudiwa!

Taarifa zinaonesha kwamba, kwa sasa Baraza la Maaskofu Katoliki Sri Lanka kwa kushirikiana na Vatican wanaendelea kukamilisha maandalizi na kwamba, ratiba kamili itakamilika baada ya ujumbe kutoka Vatican kutembelea nchini Sri Lanka mapema mwezi Novemba. Maaskofu wamekwishazungumza na vyombo vya ulinzi na usalama, ili kuhakikisha kwamba, ziara hii inafanyika katika hali ya utulivu na amani.

Mwanzoni, wananchi wengi walionesha wasi wasi wa kufanyika kwa hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu nchini Sri Lanka kutokana na maendeleo ya mchakato wa uchaguzi nchini humo, uchaguzi ambao unatarajiwa kufanyika kabla au baada ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko. Viongozi wa Kanisa wanashauri, ikiwezekana uchaguzi ufanyike baada ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu nchini Sri Lanka.







All the contents on this site are copyrighted ©.