2014-10-27 16:08:32

Lugha hutambulisha imani ya Mtu- Papa


Maneno yetu yanaweza kutangaza iwapo sisi ni Wakristo wa kweli , au ni watu wa giza au ni Wakristo nusunusu.


Ni muhimu kuchunguza dhamiri ya maneno au lugha tunayotumia katika mazungumzo kwa kuwa huonyesha hadhi na imani ya mtu, iwapo ni mtoto wa mwanga wa kweli wa Kristo , au ni mtoto wa shetani au iwapo Ukristo wetu upo nusunusu, Baba Mtakatifu Francisko alieleza katika hotuba yake mapema Asubuhi katika Kanisa dogo la Mtakatifu Marta.


Maelezo ya Papa, yalilenga katika somo kutoka barua ya Mtume Paulo kwa Waefeso , ambamo mnasema, watu huweza kutambuliwa kwa maneno yao. Papa alirejea barua hiyo na kutoa mwaliko kwa Wakristo, kutenda na kuzungumza na kuishi kama watoto wa mwanga, na si kama watoto wa giza. Maneno ya Mtume Paulo ni mafundisho ya kina, ambamo ndani mwake kuna maneno yanayoweza kutuonyesha iwapo sisi ni watoto wa giza.


Papa alieleza na kuhimiza kila mmoja kujihoji iwapo tunazungumza kinafiki kwa lengo la kuchota kidogo hapa, na pia kidogo kule na kuwa mtu wa katikati, mnafiki mchonganishi, asiyeeleweka, anasimama upande gani. Papa alihoji kuwa mtu wa aina hiyo kumfaa nini mtu? Aliitaja tabia hiyo kuwa ni unafiki mtupu. Alindelea kukemea mazoea ya kutoa matusi na kudhihaki wengine, kuwa na maneno yasiyo faa, maneno yasiyokuwa na maana yenye kusababisha migogoro hata kwa mambo madogomadogo yasiyokuwa na maana,. Lugha Chafu, daima haijengi bali huboa na ni ubatili mtupu na upuuzi mtupu.


Papa amesema, lugha chafu si lugha ya watoto wa mwanga , wala si kutoka kwa Roho Mtakatifu, na wala si kutoka Yesu, watu hao si wana wa Injili ... njia hiyo ya kuzungumza, daima juu ya mambo machafu huongoza katika kuyapenda ya dunia na mambo yake ya kibatili na unafiki.


Basi, ni yapi maneno ya Watakatifu, au ya watoto wa mwanga wa Kristo?

Papa Francisko alitoa ufafanuzi kwa kurejea barua za Mtakatifu Paulo ambamo anasema, Igeni Mungu, kutembea katika upendo, kutembea katika wema, kutembea katika upole, kwa kuwa wale wanaotembea katika njia hii ....hujaliwa neema ya huruma. Mtume Paulo anasema, kusameheana kama Mungu alivyowasamehe ninyi pia katika Kristo. Basi, wafuasi wa Mungu hutembea katika upendo , yaani, kutembea katika huruma, msamaha na upendo.Hayo ndiyo maneno ya mtoto wa mwanga. Hao ni Wakristo thabiti walio katika mwanga kamili, alibainisha Papa - ambao wanataka kumtumikia Bwana katika mwanga huu.


Papa pia alieleza juu ya kundi jingine kundi la Wakristo wanaoishi katika giza, ambao maisha yao yanaongoza katika kutenda dhambi, maisha ya kuwa mbali na Bwana na ambao lugha yao huwaonyesha kuwa mbali na Kristo. Watu waliojitenga na kanisa na kuyakumbatia ya dunia hii.


Aidha Papa, alizungumzia kundi la tatu la Wakristo", ambao si mwanga wala giza, akiwataja kuwa wao ni Wakristo walio katikati, maisha yao hayajulikani wako kundi gani, iwapo ni Wakristo au la. Hawa ni Wakristo wa rangi ya kijivu si nyeupe wala nyeusi wako tu hapo, haijulikani kama ni watu wa Mungu au ni wafuasi wa shetani. Papa alionya kwamba, Mungu hapendi watu wa aina hiyo. Watu wasiokuwa na maamuzi thabiti katika maisha. Alieleza kwa kurejea kaitkakitabu cha Ufunuo,ambamo Bwana anasema, kwa kuwa wewe ni si moto wala baridi nitakutapika kutoka kinywa changu .. Ni maneno ya kutisha kutoka kwa Bwana, kwa ajili ya Wakristo hao walio katika eneo la uvuguvugu, wenye kusema Mimi ni Mkristo, lakini hawaonyeshi lolote katika Ukristo wao . Maneno na vitendo vyao huwa na madhara makubwa, kwa sababu ushahidi wao kama Wakristo huishia kupanda mbegu isiyoeleweka , na mara nyingi hupandikiza fujo na ushahidi hasi.


Papa alihitimisha homilia yake kwa kuhimiza kuishi kama watoto wa mwanga. Na kwamba, watu wote inafaa kutafakari vyema, iwapo maneno na matendo yetu, yanatoa miali ya mwanga wa mwanga wa Kristo, au iwapo tu wakristo wa giza?au tu Wakristo wa uvuguvugu, tusiojulikana tuko wapo, Mkristo wa katikati?

Papa ametoa mwaliko kwa watu wote, kuchukua hatua za mbele katika kuwa na mwanga wa kukutana na Bwana.











All the contents on this site are copyrighted ©.