Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na taasisi mbili kubwa za kimataifa Jumapili,
Oktoba 26, 2014, zilitiliana saini Hati ya Makubaliano (MOU) ya kuendeleza kwa pamoja
Eneo la Kiuchumi la Bagamoyo ambako pia itajengwa bandari kubwa ya Bagamoyo ambayo
inatarajiwa kutoa mchango mkubwa kwa uchumi wa Tanzania.
Pande hizo tatu ambazo
ni pamoja na Kampuni ya Uendeshaji Bandari ya China Merchant Holding International
(CMHI) ya Jamhuri ya Watu wa China na Mfuko wa Uwekezaji wa Oman wa State General
Reserve Fund of Oman ya Oman zimetilia saini Hati hiyo kwenye sherehe iliyofanyika
katika Hoteli ya Hilton Shenzhen Shekou Nahai ya mjini Shenzhen, Kusini mwa China.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye ametembelea
Jimbo la Guang Dong ambako liko Eneo la Uwekezaji wa Kiuchumi la Shenzhen alishuhudia
utiaji saini huo ambao kwa upande wa Tanzania saini ilitiwa na Katibu Mkuu wa Wizara
ya Fedha, Dkt. Servicus Likwelile. Chini ya Hati hiyo ya uendelezaji wa Eneo la Uwekezaji
la Bagamoyo litaanza kujengwa Julai Mosi mwakani, 2015.
Kabla ya sherehe hiyo
ya kutiliana saini Hati ya Makubaliano, Rais Kikwete ametembelea Eneo la Kontena la
Bandari ya Shenzhen ambako alionyeshwa vifaa vya kisasa kabisa vya kupakia na kupakulia
kontena kazi inayofanywa na CMHI ambayo ina uzoefu wa miaka 140 wa uendeshaji wa bandari.
Akizungumza
katika sherehe hiyo, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake imedhamiria kuhakikisha
kuwa mradi huo wa mamilioni ya fedha wa Bangamoyo unaanza. “Tutafanya lolote linalowezekana
kuhakikisha kuwa mradi huu unaanza kwa sababu utaleta neema kubwa ya kiuchumi kwa
nchi nzima.”
Naye Mwenyekiti wa CMHI, Bwana Li Jianhong ameitaka Serikali kuangalia
uwezekano wa kumaliza vikwazo vyote ambavyo vimechelewesha kuanzishwa kwa mradi huo
ili uweze kuanza Julai Mosi, mwakani, kama ilivyokubaliwa.
Mapema siku ya Jumapili
akiwa Shenzhen, Rais Kikwete ametembelea makao makuu ya Kampuni ya Teknolojia ya Mawasiliano
ya Hauwei Technologies inayoajiri maelfu ya watu duniani, ikiwemo Tanzania, na kutengeneza
mamilioni ya faida. Aidha, Rais Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi
wa Manispaa ya Shenzhen ambayo yalifanyika kwenye hoteli ambako alifikia Rais Kikwete
katika ziara yake ya Shenzhen ya Shenzhen Wazhou Guest Hotel ambayo ni mali ya Serikali
ya China. Rais pia ametembelea Makao Makuu ya Kampuni ya Teknolojia ya Mawasiliano
ya ZTE iliyoko mjini Shenzhen ambayo inaendesha shughuli zake Tanzania na inaajiri
wafanyakazi 60,000 dunia nzima.
JK Rais wa kwanza kupokelewa kwa pikipiki
China kwa miaka 10 iliyopita!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesababisha mageuzi makubwa kwa namna Jamhuri ya
Watu wa China inavyowapokea viongozi wageni kutoka nje kwa kuwa kiongozi wa kwanza
duniani kupokewa rasmi na pikipiki za Polisi na kuongozwa na pikipiki hizo kwa muda
wote wa ziara katika kipindi cha miaka 10 iliyopita.
Rais Kikwete ambaye aliwasili
nchini China Jumanne iliyopita, Oktoba 21, 2014, kuanza ziara rasmi ya siku sita nchini
humo, amekuwa kiongozi wa kwanza wa nje kupokelewa na msafara wa pikipiki tokea Januari
Mosi, mwaka 2004, miaka 10 iliyopita wakati China ilipofuta utaratibu wa misafara
ya viongozi kusindikizwa na pikipiki za Polisi.
Rais Kikwete na msafara wake
alipokewa na msafara wa pikipiki wa polisi mara baada ya kuwasili Uwanja wa Ndege
wa Beijing hadi kwenye Nyumba ya Kufikia Wageni wa Serikali ya Diaoyutai, katikati
ya Jiji la Beijing na utaratibu huo kuendelea kuongoza msafara wake kwa siku zote
alipokuwa China. Taarifa ya habari iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya China
na kukaririwa na Shirika la Habari la nchi hiyo la Xinhua haikutoa sababu zozote za
mabadiliko ya sera hiyo.
Katika nchi karibu zote duniani, utaratibu wa viongozi
wa nchi mbali mbali kupokelewa kwa misafara ya pikipiki ni protokali ya juu kabisa
ambayo pia huongeza usalama wa kiongozi na ni utaratibu wa kawaida katika nchi nyingi
duniani. Tokea kuasisiwa kwake mwaka 1949, Jamhuri ya Watu wa China ilikuwa na utaratibu
wa pikipiki za polisi kuongoza misafara ya viongozi lakini utaratibu huo ulisimamishwa
Januari Mosi, mwaka 2004, kwa sababu ambazo hazijapata kuelezwa.