Zambia inaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wake kwa kupata Rasimu ya Katiba
Mpya!
Jukwaa la Wakristo nchini Zambia linaloungayaunganisha Mabaraza mbali mbali ya Makanisa
nchini Zambia, katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Zambia ilipojitwalia
uhuru wake kutoka kwa Mwingireza hapo tarehe 24 Oktoba 1964, limeandika ujumbe unaowapongeza
wananchi wa Zambia kwa kuendelea kudumisha amani na umoja wa kitaifa, licha ya misukosuko
mbali mbali iliyojitokeza nchini humo katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.
Jubilee
ni kipindi cha kumshukuru Mungu na kufanya tafakari ya kina kuhusu mapungufu ili kuweza
kuyarekebisha kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa wananchi wa Zambia kwa siku za usoni.
Kwa kipindi cha miaka 50 iliyopita, Serikali na Kanisa kwa pamoja wameshikamana katika
kuwahudumia wananchi wa Zambia katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu.
Ni matumaini ya Jukwaa la Wakristo kwamba, kwa pamoja wataendelea kujenga na kudumisha
misingi ya haki, amani na mshikamano wa kitaifa.
Zambia imeonesha maendeleo
kidogo katika masuala ya mfumo wa vyama vingi vya kisiasa; nchi imeendelea kuwa ni
makazi ya wakimbizi na wahamiaji waliokuwa wanatafuta hifadhi na usalama wa maisha
yao na kwamba, kumekuwepo na maendeleo makubwa yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho
na kimwili, ingawa changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, kuna kuwepo na
mgawanyo bora zaidi wa huduma na raslimali ya nchi ya Zambia kwa watu wake wote, ili
maendeleo ya kiuchumi na kijamii yaweze kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Rasilimali
ya nchi haina budi kutumika kwa kuzingatia misingi ya haki, usawa na utawala bora,
mambo ambayo bado yanapaswa kufanyiwa kazi kwa siku za usoni. Zambia imeendelea kubeba
mzigo wa deni kubwa la ndani na nje ya nchi katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita,
zigo linalowaelemea wananchi wa Zambia, changamoto ya kuwa na matumizi bora na sahihi
ya fedha za umma, sera na utekelezaji makini kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi
wa Zambia.
Zambia kwa siku za usoni, haina budi kujikita katika mchakato wa
kukuza na kudumisha haki jamii, mafao ya wengi na sera za maendeleo endelevu kwa wananchi
wote, kwa kujikita katika misingi ya upendo, ukweli, umoja, ukarimu, uwajibikaji na
mshikamano wa dhati, ili kweli Zambia iweze kuwa ni nchi moja si tu kwa maneno bali
kwa njia ya ushuhuda wa maisha.
Umaskini unaendelea kuwaelemea wananchi wengi
wa Zambia wanaoishi mijini, lakini zaidi wale wanaoishi vijijini, changamoto kwa Serikali
na wadau mbali mbali kujifunga kibwebwe kupambana na umaskini.
Zambia inaadhimisha
Jubilee ya miaka 50 ya uhuru wake, ikimshukuru Mungu kwa kupata Rasimu ya Katiba Mpya,
ambayo imewatesa sana wananchi wa Zambia kiasi hata cha kutishia usalama, umoja, mshikamano
na mustakabali wa wananchi wa Zambia. NI matumaini ya Jukwaa la Wakristo kwamba, Serikali
ya Zambia itaonesha ratiba ya mchakato wa kupata Katiba Mpya ya Zambia.
Wananchi
waelimishwe umuhimu wa kushiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii, huku wakidumisha:
haki na amani. Mashirika ya misaada yatumie fursa na rasilimali zake katika kupambana
na umaskini nchini Zambia. Wanavishukuru vyombo vya habari nchini Zambia kwa kusaidia
kuwahabarisha wananchi wa Zambia.
Ujumbe huu umehaririwa na Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican