2014-10-23 11:09:44

Jitoeni kimasomaso kuonesha upendo kwa Mungu na jirani!


Roho Mtakatifu anawawezesha Wakristo kupata nguvu ya kupenda na kujitosa kimasomaso bila ya kujibakiza kama alivyofanya Mtakatifu Paulo katika barua yake kwa Waefeso, kwa kuwashirikisha uzoefu na mang'amuzi ambayo yalimfanya kuacha yote, kwa vile alitaka kuonesha upendo wa dhati kabisa kwa Kristo.

Hiki ni kielelezo makini cha mtu anaye abudu kwa kumpigia Mwenyezi Mungu magoti, kwa kutambua kwamba, ana uwezo wa kufanya mambo mengi hata yale ambayo mwanadamu athubutu kuomba mbele ya Mwenyezi Mungu.

Hayo yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokuwa anatoa mahubiri kwenye Ibada ya Misa Takatifu, kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Siku ya Alhamisi asubuhi tarehe 23 Oktoba 2014

Mtakatifu Paulo anawaalika waamini kumwabudu Mwenyezi Mungu na kumpenda bila kikomo na anawaombea ili kweli waweze kuimarishwa katika utu wao wa ndani kwa njia ya Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu anawaimarisha waamini na kuwapatia nguvu ya kusonga mbele kwa imani na matumaini, kwa kutambua kwamba, kutokana na unyonge wao wa kibinadamu, wakati mwingine wanakosa nguvu na ujasiri. Ni kwa njia ya neema ya Roho Mtakatifu watu wanawezeshwa kuwa ni Wakristo, tayari kusonga mbele katika utekelezaji wa Amri za Mungu.

Mtakatifu Paulo anawaombea Wakristo neema na baraka kutoka kwa Yesu Kristo, ili awawezeshe kukua na kukomaa katika upendo wa Kristo usiokuwa na mipaka, unaoonesha ukuu wa Mungu. Haya ndiyo mang'amuzi ya Mtakatifu Paulo kuhusu: Sala ya kusifu na kuabudu dhidi ya mapungufu yanayoweza kujitokeza kwa waamini wakati wa sala. Roho Mtakatifu anawawezesha waamini kusonga mbele kwa kufarijika na kujizamisha katika upendo unaobubujika kutoka kwa Yesu Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha mahubiri yake kwa kusema kwamba, huu ndio msingi wa maisha ya kiroho, unaomwezesha mwamini kutambua jinsi ambavyo Mtakatifu Paulo alivyoacha yote, ili aweze kumpata Kristo na baadaye kupata yote ndani ya Kristo. Ni ajabu ya kupendeza kumsifu na kumtukuza Mwenyezi Mungu, kwa kuwagawia wengine upendo na ukarimu unaobubujika kutoka kwa Yesu Kristo. Kwa njia hii, waamini wanaweza kusonga mbele katika mchakato wa kumwilisha ile Amri kuu ya mapendo kwa Mungu na jirani.







All the contents on this site are copyrighted ©.