2014-10-23 08:37:11

Endeleeni kusali na kuchangia mawazo kwa ajili ya maadhimisho ya Sinodi ya Familia kwa Mwaka 2015


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, wakati wa maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia iliyofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe 5 ahdi tarehe 19 Oktoba 2014, ilikuwa ni fursa kwa Mama Kanisa kusikiliza kwa makini ushuhuda na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza katika maisha na utume wa Familia. Kanisa limemwangalia Kristo, ili liendelee kutangaza Injili ya Familia kwa Watu wa Mataifa, huku likikabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wa Familia. RealAudioMP3

Askofu Ngalalekumtwa ambaye alikuwa analiwakilisha Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika maadhimisho ya Sinodi hii anasema kwamba, awamu ya kwanza imehitimishwa na hati ya Mababa wa Sinodi itakuwa ni mwongozo na rejea katika kujiaandaa kwa ajili ya maadhimisho ya awamu ya pili ya Sinodi itakayofanyika kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015 kwa kuongozwa na kauli mbiu "Wito na utume wa Familia katika Kanisa na Ulimwengu mamboleo". Mababa wa Sinodi wametafakari kwa kina na mapana baraka ya maisha ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu.

Askofu Ngalalekumtwa anasema wanandoa watarajiwa wanahaki ya kuandaliwa vyema ili waweze kutambua dhamana na utume wao katika Kanisa. Wanapofunga ndoa, wasindikizwe kwa hekima na busara, ili kuendelea kupyaisha upendo wa maisha ya ndoa na familia. Wanandoa wanapaswa kujiandaa kikamilifu: kiakili, kiroho na kijamii ili kuipokea Sakramenti ya Ndoa kwa imani na matumaini na hatimaye kufurahia baraka ya ndoa.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, kwa hakika ndoa inahitaji malezi endelevu, ili kuimarisha kifungu cha upendo na mshikamano wa dhati. Kinzani, migogoro na hatimaye talaka ni dalili za kuanza kuporomoka ile neema ya maisha ya ndoa na familia. Wanandoa wanakumbushwa kwamba, wao ni kielelezo cha upendo wa Kristo kwa Kanisa lake. Kristo anaendelea kulipenda Kanisa licha ya mapungufu yanayofanywa na watoto wake.

Tangu sasa waamini waendelee kusali kwa ajili ya Sinodi, wakitafakari na kuchangia mawazo kuanzia katika familia, Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo, Vigango, Parokia, Majimbo hadi ngazi ya kitaifa na kikanda, ili Kanisa liweze kutambua matatizo, changamoto na fursa zilizopo kama sehemu ya utekelezaji wa mchakato wa kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Familia. Kanisa linawahitaji watu wenye msimamo thabiti katika maisha na kwamba, mchango wa waamini utawawezesha Mababa wa Kanisa kutambua makali yanayozikabili familia!







All the contents on this site are copyrighted ©.