2014-10-21 07:45:51

Kanisa linahitaji rasilimali watu, vitu na fedha katika kazi ya Uinjilishaji!


Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari katika mahojiano maalum na Radio Vatican wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimissionari Duniani, iliyoadhimishwa Jumapili iliyopita, tarehe 19 Oktoba 2014 anasema kwamba, Kanisa linahitaji rasilimali watu, vitu na fedha kwa ajili ya kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Ni jukumu la waamini katika Makanisa mahalia kuanza kujiwekea mikakati ya kulitegemeza Kanisa, ili liweze kutekeleza vyema utume wake kati ya watu. Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari yalianzishwa na Mama Kanisa, ili kuwahamasisha waamini kushiriki kikamilifu katika kuchangia rasilimali watu, fedha na vitu katika kuendeleza kazi ya Uinjilishaji hadi miisho ya dunia, sanjari na kuonesha mshikamano wa hali na mali na Makanisa mahalia.

Askofu mkuu Rugambwa anasema kwamba, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaalikwa kuchangia katika mfuko wa jumla wa shughuli za Uinjilishaji, ili kuyawezesha Makanisa machanga kuendeleza dhamana na utume wa kuwatangazia Watu wa Mataifa Injili ya Wokovu, wakidhihirisha matendo makuu ya Mungu katika maisha ya mwanadamu. Huu ni wajibu wa kila mwamini, lakini pia waamini wanapaswa kuhamasishwa na kuelimishwa kuhusu ushiriki wao katika kuchangia utume wa Uinjilishaji.

Askofu mkuu Protase Rugambwa anasema sadaka na majitoleo haya ni muhimu sana katika kulitegemeza Kanisa mahalia sanjari na kushiriki katika kuendeleza kazi ya Uinjilishaji inayohitaji rasilimali watu, vitu na fedha.







All the contents on this site are copyrighted ©.