Jengeni utamaduni wa mshikamano unaojikita katika misingi ya haki na amani!
Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini limewaandikia ujumbe waamini wa dini ya
Kihindu kwa ajili ya Siku kuu ya Mwanga kama inavyojulikana "Deepavali" inayoadhimishwa
tarehe 23 Oktoba 2014, ili mwanga kutoka juu, uweze kuwaangazia wao na majirani zao,
ili kujenga na kudumisha utulivu, furaha, amani na maendeleo, kwa kujikita kwa pamoja
katika utamaduni unaowakumbatia wote bila ya ubaguzi. Tema ya ushirikishwaji ni muhimu
sana kwa watu wa nyakati hizi ambao wanakumbana na mifumo mbali mbali ya ubaguzi na
kinzani.
Ni ukweli kwamba, utandawazi umefungua mipaka na kutoa fursa za maendeleo
makubwa katika sekta ya elimu na afya. Umesaidia kukuza na kudumisha uelewa mkubwa
wa demokrasia na haki jamii katika ulimwengu huu ambao kwa sasa unaonekana kama ulimwengu
kijiji kutokana na maboresho ya njia za mawasiliano na usafiri. Kwa hakika mchakato
wa utandawazi haujafanikiwa kufikia lengo la kuwajumuisha watu mahalia katika Jumuiya
ya Kiulimwengu na matokeo, imechangia kuwafanya watu wengi kupoteza utambulisho wao
wa kijamii na kitamaduni; kiuchumi na kisiasa.
Utandawazi umekuwa na athari
kubwa hata katika Jumuiya za kidini kwani hata hizi pia ziko duniani. Jamii nyingi
zimemeguka na hivyo kusababisha ubinafsi na mawazo mepesi mepesi kutawala, kiasi cha
kuifanya dini kuwa ni jambo binafsi lisilokuwa na mvuto wala mguso kwa Jamii husika.
Kumekuwepo na ongezeko la misimamo mikali ya kidini na kiimani pamoja na ukabila,
mambo yanayokatisha tamaa; ongezeko la wasi wasi kuhusu usalama miongoni mwa Jamii,
lakini zaidi kati ya maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kundi
ambalo bado halijafaidika na fursa za utandawazi.
Utandawazi umechochea ulaji
wa kupindukia na tabia ya watu kupenda mali na hivyo kumezwa na malimwengu. Ubinafsi,
uchu wa mali na madaraka; ukosefu wa haki msingi pamoja na baadhi ya watu ndani ya
Jamii kusababisha mateso kwa jirani zao. Huu ndio utandawazi usiojali wala kuguswa
na mahangaiko ya wengine kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko. Ulimwengu mamboleo
unasheheni kundi kubwa la maskini ambao wananyimwa haki zao msingi; fursa na rasilimali
ambayo inapatikana kwa wanajamii wengine. Kundi hili linaonekana kuwa ni mzigo wa
Kijamii, kundi lisilopendwa wala kuthaminiwa.
Katika mfumo kama huu wa maisha,
kuna watoto na wanawake wanaonyanyaswa; wazee wasiotunzwa wala kuheshimiwa, wagonjwa,
walemavu, wahamiaji na wakimbizi; kuna makundi ya waamini yanayoendelea kudhulumiwa
kutokana na imani yao; mambo yote haya ni kielelezo cha kukua na kukomaa kwa utamaduni
wa ubaguzi.
Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini linasema, mchakato wa
ujenzi wa utamaduni wa mshikamano ni mwaliko kwa wote, unaojikita katika uwajibikaji
wa pamoja unaopaswa kufanyiwa kazi. Huu ni mradi unaopania kutunza afya na ustawi
wa Familia ya binadamu licha ya nguvu ya utamaduni wa ubaguzi inayoendelea kutikisa
maisha ya mwanadamu kwa nyakati hizi. Wakristo na Wahindu kwa kushirikiana na waamini
wa dini mbali mbali wanaweza kujenga utamaduni wa mshikamano ili kujenga jamii inayosimikwa
katika msingi wa haki na amani.