Hati ya Mababa wa Sinodi maalum kuhusu Familia imechapishwa!
Baba Mtakatifu Francisko ameridhia kuchapishwa kwa Hati ya Mababa wa Sinodi ambayo
ni mkusanyiko wa mawazo ya wajumbe binafsi na yale yaliyokusanywa katika majadiliano
ya vikundi; hati ambayo kwa lugha ya kitaalam inajulikana kama "Relatio Synodi".
Hiki
ni kielelezo cha ukweli na uwazi, ili kuonesha ni wapi ambapo Mababa wa Sinodi wamekubaliana
kimsingi na pale ambapo wameonesha kugawanyika kutokana na mitazamo na tamaduni za
watu. Mababa wa Sinodi waliweza kufanya marekebisho 470 yaliyowasilishwa kwenye vikundi
vidogo vidogo kutoka kwenye Hati Elekezi iliyotolewa mara tu baada ya maadhimisho
ya Sinodi katika Juma la kwanza la kazi.
Hati ya Mababa wa Sinodi sehemu ya
kwanza inaonesha: Umuhimu wa Kanisa kusikiliza: mintarafu mazingira na changamoto
za maisha ya kifamilia: Hapa Mababa wa Sinodi wanaangalia mazingira ya kijamii na
kitamaduni; umuhimu wa hisia katika maisha ya watu pamoja na changamoto za kichungaji
zinazoendelea kujitokeza ndani ya Kanisa.
Sehemu ya Pili ya hati hii, inamwangalia
Kristo, ili kuliwezesha Kanisa kutangaza Injili ya Familia. Hapa Mababa wa Sinodi
wanaelezea mpango wa Mungu katika historia ya ukombozi; familia kama kielelezo makini
cha mpango wa ukombozi. Mababa wanaangalia familia kama ilivyojadiliwa katika Nyaraka
mbali mbali za Kanisa.
Wanatambua kwamba, kiini cha Sakramenti ya ndoa ni
upendo usiogawanyika na kwamba, ndoa ni zawadi ya kudumu ambayo inawaalika wanandoa
kuifurahia kwa kuishi kwa pamoja. Wanandoa wanapaswa kutambua kweli na uzuri wa maisha
ya ndoa na familia kwa kuendelea kujikita katika huruma ya Mungu ili kuponya madonda
na mapungufu yanayojitokeza katika maisha ya binadamu.
Sehemu ya tatu ya Hati
ya Mababa wa Sinodi inapembua kwa kina na mapana mikakati ya kichungaji, ili kuliwezesha
Kanisa kutangaza Injili ya Familia katika ulimwengu mamboleo na kati ya watu wanaoishi
katika mazingira tofauti. Mababa wa Sinodi wanaliomba Kanisa kuwasindikiza kwa moyo
wa unyenyekevu wanandoa watarajiwa katika mchakato wa maandalizi ya ndoa; kuendelea
pia kuwasindikiza katika maisha haya katika miaka yao ya kwanza kwanza ya maisha ya
ndoa na familia.
Kanisa halina budi kubainisha mikakati ya kichungaji kwa
ajili ya wale waliofunga ndoa Serikalini na wale ambao bado wanaishi "uchumba sugu".
Mababa wa Sinodi wanasema, Kanisa lisaidie kutibu madonda ya wanandoa waliotengana
na kuamua kuoa au kuolewa tena; familia tenge, yaani zinazosimamiwa na mzazi wa upande
mmoja.
Kanisa lioneshe jicho la huruma kwa watu wenye mielekeo ya kuwa na
mahusiano ya jinsia moja. Mama Kanisa anapenda kukazia umuhimu wa familia kurithisha
zawadi ya maisha na changamoto zilizopo katika kupanga uzazi. Mwishoni, Mababa wa
Sinodi wanaangalia changamoto ya elimu na dhamana ya Familia katika Uinjilishaji.
Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anasema kwamba, vipengele
vyote sitini na viwili, vilipigiwa kura na Mababa wa Sinodi 183. Kati ya vipengele
hivi, pendekezo la wanandoa waliotalakiana na hatimaye kuamua kuoa au kuolewa kushiriki
katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, halikuungwa mkono na Mababa wengi wa Sinodi
na limeamriwa kwamba, litajadiliwa kwa kina wakati wa Maadhimisho ya Sinodi ya kawaida
ya Maaskofu, hapo Oktoba, 2015. Mababa wa Sinodi wamekataa kufananisha ndoa za watu
wa jinsia moja na Sakramenti ya ndoa.