2014-10-16 08:46:46

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 29 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa


Karibuni mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican tusafiri pamoja katika kuumega mkate, ndiyo Neno la Mungu, chakula cha roho zetu. Ni Dominika ya 29 ya mwaka A wa Kanisa. Mpendwa, ujumbe wa tafakari yetu ni utambuzi wa namna gani mwamini mkristu aweze kuishi ukristu wake katika maisha ya kawaida ya kijamii, akishiriki mambo yote bila kuharibu mpango wa Mungu, na hivi kumbe kuingiza daima chachu ya Injili katika maisha ya kidunia. RealAudioMP3

Katika somo la kwanza tunamwona nabii Isaya akitafakari mpango wa Mungu ulio wa ajabu. Wakati Waisraeli wamekata tamaa, Mungu anamtuma mfalme mpagani wa Persia yaani Koreshi ambaye ataiteka Babilonia na baadaye atawaweka huru Waisraeli warudi nyumbani. Ataruhusu tena mahekalu yaliyobomolewa na Wababilonia yajengwe na kila mmoja ataruhusiwa kushiriki dini yake katika uhuru.

Nabii Isaya anatafsiri hali hii, kuwa ni mpango wa Mungu wa wokovu kwa taifa la Israeli. Anamwona huyu Koreshi kama mchungaji, mtu aliyeletwa na Mungu, mpendwa wa Mungu. Anaonekana kama masiha lakini nabii Isaya haoneshi kuwa yeye ndiye mfalme wa Israeli atakayekuja kwa ajili ya ukombozi wa Israeli. Ni chombo cha Mungu kwa kuondolewa utumwani huko Babeli.

Mpendwa, mara kadhaa tuko utumwani hapa nchini petu, kijijini petu, je tunaona alama za nyakati ambazo Mungu huweka katikati yetu akituonesha kuwa yu pamoja nasi katika shida zetu na hivi katika yeye twaweza kuondolewa katika shida hizo? Ninachotaka kukuambia ni hiki, kuza moyo na macho yako ili daima uone mpango wa Mungu maishani mwako kila siku katika kile tunachokiita alama za nyakati!

Mpendwa msikilizaji, ni kwa njia ya sala na kuombeana kijumuiya twaweza pia kuona mpango wa Mungu. Si sala na maombi tu bali kurutubisha na kudumu katika imani tuliyoipokea wakati wa ubatizo kwa majitoleo mengine yampendezayo Mungu. Jambo hili linasisitizwa na Mtume Paulo kwa Watesalonike akiwaambia kuwa anawakumbuka kwa sala na kuwapongeza kwa maana kile alicho kisia kinakua na kuzaa matunda ndiyo upendo na moyo wa kuikuza imani katika Yesu Kristu na sasa anataka wadumu katika imani bila kurudi nyuma.

Katika Injili ya leo kutoka mwinjili Mathayo tunajifunza kuwa Imani ni jambo ambalo hatuwezi kuliishi nje ya dunia hii, yaani bila uhusiano na shughuli za kijamii. Mtu aliye mkristu anaishi katika jamii ya watu. Imani si jambo la siri wala la muda mfupi bali ni jambo la wazi kabisa na la muda wote. Ni kwa jinsi hii dini hujikita katika maisha ya kawaida ya kijamii na kisiasa na humdai mtu kushiriki kazi zote za kijamii. Kila Mkristu yampasa kuchangia maendeleo ya mwanadamu na jamii kwa ujumla na zaidi kuwa mfano bora kwa wengine.

Katika Injili ya Dominika hii ya 29 kielelezo msingi cha kuwajibika kijamii kinatujia kwa sura ya kodi kwa Kaisari. Kumbe ni vema na ni lazima na muhimu kulipa kodi au tuseme kuwapo pamoja na wengine katika kusimamia mambo yahusuyo haki na amani katika jumuiya, lakini pia tunao wajibu wa kuhoji hiyo kodi inatumikaje na hivi kusukuma mbele lengo lake liweze kufikiwa bila kuharibu utulivu wa jamii husika. Ndiyo kusema tunapaswa kuingiza chachu ya Injili katika maisha ya jamii (Rejea Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, GS)

Tunapozungumza ya Mungu mpe Mungu tunataka kusema yale yote ambayo ametuagiza tuyafanye kwa sifa na utukufu wake lazima tuyafanye kwa unyenyekevu, kwa upendo na ufasaha. Injili inatupa fundisho zuri kweli nalo ni hili: mpende Mungu kwa akili yako yote, kwa moyo wako wote na kwa roho yako yote na kisha jirani yako!

Jirani ni mwanadamu mwenzako ambaye ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Huyu jirani ndiye unapaswa kumrudishia Mungu, ndiyo yaliyo ya Mungu. Jirani huyu ndiye ambaye unakutana naye ofisini, katika siasa na katika familia. Kumbe, tengeneza maisha ya kijamii yaliyo mazuri na hivi mwanadamu atainuliwa juu katika utu wake na Mungu ataisifiwa katika mwanadamu huyu na hivi wajibu wako wa kumpa Kaisari yaliyo yake na Mungu yaliyo yake utakuwa si wajibu pinzani bali wajibu mwafaka kwa wokovu wako.

Fundisho hili latupa changamoto ya kuheshimu wanadamu wote na hivi polepole kukua katika kutambua chanzo chao ambacho ni Mungu. Viongozi wote wa uma kumbukeni wajibu huu daima ili kusudi kazi ya kuongoza isiwe chanzo cha kupotea bali utumishi mtakatifu utakaokuletea wokovu.

Tumsifu Yesu Kristu na Maria. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.