2014-10-16 11:39:21

Familia zinasubiri ujumbe wa matumaini!


Baada ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia iliyokuwa inafanyika katika makundi madogo madogo katika vikao vyake saba, Alhamisi tarehe 16 Oktoba 2014, Mababa wa Sinodi wamepokea taarifa za vikundi na kuanza kuifanyia kazi kwa kusikiliza mchango kutoka kwa Mababa wa Sinodi.

Mchango wa makundi baada ya kukamilika, utakuwa ndio matunda ya kazi ya Mababa wa Sinodi, inayojulikana kwa lugha ya Kilatini "Relatio Synodi" kama alivyobainisha Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Vatican kuhusiana na Sinodi. Hati ya Mababa wa Sinodi itawakilishwa kwa Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 18 Oktoba, tayari kufanyiwa kazi.

Kardinali Lluis Martines Sistach anasema, majadiliano kwenye makundi yamefanyika katika misingi ya umoja na mshikamano; udugu pamoja na kuzingatia changamoto za kichungaji. Mababa wa Sinodi wameonesha uhuru na ukomavu, ukweli na uwazi katika kujadili hata zile mada tete, kwa kutambua kwamba, kuna changamoto za kichungaji zilizoko mbele yao zinazopaswa kufanyiwa kazi.

Kardinali Joseph Edward Kurtz kwa upande wake anasema, Mababa wa Sinodi wamezungumza kwa uhuru wakiwa na nia moja katika majadiliano, kwa kuheshimiana na kuthaminiana, ili kuliwezesha Kanisa kutoa mwelekeo chanya wa kimissionari na ujumbe wa matumaini pasi na kukata wala kujikatia tamaa.

Askofu mkuu Rino Fisichella anasema, matatizo na changamoto za kifamilia ni kielelezo cha mtikisiko wa imani, pale ambapo familia zinajikita katika imani thabiti, hapo hakuna cheche za kinzani katika tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.







All the contents on this site are copyrighted ©.