2014-10-15 09:02:22

Mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ebola!


Shirika la Afya Duniani, WHO, linasema kwamba, kasi ya maambukizo ya ugonjwa wa Ebola huko Afrika Magharibi inaweza kuongezeka maradufu hadi kufikia wagonjwa 10, 000 kwa juma katika kipindi cha miezi miwili kuanzia sasa. Ugonjwa huu umekwisha sababisha vifo vya watu 4, 500 wengi wao wakiwa ni wagonjwa kutoka Afrika Magharibi.

Hii ni changamoto kubwa ambayo inapaswa kufanyiwa kazi na Umoja wa Mataifa kabla mambo hayajaharibika zaidi. Lengo ni kuhakikisha kwamba, kunakuwepo walau vijana 7, 000 kwa ajili ya kutolea tiba kwa wagonjwa na kikosi kazi cha watu 500 kitakachoshughulikia maziko ya wagonjwa watakaofariki kwa Ebola. Rais Barack Obama wa Marekani akizungumza na viongozi wa kijeshi kutoka Marekani na Washirika wake amebainisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa bado haijauvalia njuga ugonjwa wa Ebola.

Wakari huo huo, Serikali ya Uingereza imetuma Meli ya Kijeshi ikiwa imesheheni watu 400 kati yao wakiwa ni wanajeshi, waganga na wauguzi kwenda Siera Leone ili kusaidia mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ebola nchini humo. Liberia na Guinea ni kati ya nchi za Afrika magharibi zilizoathirika zaidi kwa ugonjwa wa Ebola.







All the contents on this site are copyrighted ©.