2014-10-15 11:06:13

Changamoto za kichungaji katika maisha ya ndoa na familia!


Mababa wa Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia wanakiri kwamba kuna matatizo makubwa, changamoto na fursa mbali mbali katika kutangaza Injili ya Familia kwa Watu wa Mataifa. Mababa wa Sinodi wamekumbusha kwamba, Kanisa ni nyumba inayopaswa kuwakaribisha watu wote hata wale wanaoishi katika mwelekeo wa ndoa za jinsia moja bila kuhatarisha mafundisho tanzu ya Kanisa Katoliki kuhusu ndoa na familia.

Ieleweke kwamba, Kanisa halijaruhusu wala kuridhia ndoa za watu wa jinsia moja kama inavyosomeka kwenye vyombo mbali mbali vya habari!

Askofu mkuu Ignatius Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria katika mahojiano maalum na Radio Vatican anafafanua kwamba, changamoto kubwa kwa Kanisa Barani Afrika ni ndoa za wake wengi, ndoa za mseto, umaskini, ukosefu wa fursa za ajira kwa vijana. Pale ambapo kuna msingi thabiti wa ndoa, hapo familia inakuwa kweli ni chombo cha ushuhuda wa imani tendaji na sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya.

Askofu Kaigama anasema, ndoa za wake wengi ni changamoto kubwa ya kichungaji kwa Kanisa Barani Afrika. Kuna baadhi ya watu wanatamani kuwa kweli ni waamini wa Kanisa Katoliki, lakini wanajikuta wakiwa na kikwazo hiki cha wake wengi. Ndiyo maana kwa hekima na busara Mababa wa Sinodi maalum ya Maaskofu wanayaalika Makanisa mahalia kuendeleza majadiliano ya kina yatakayowawezesha Mababa wa Sinodi kuibuka na mbinu mkakati wa kichungaji wakati wa maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Familia itakayoadhimishwa mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015.

Ndoa za mseto ni changamoto nyingine hasa pale inaposhikamanishwa na misimamo mikali ya kiimani kama inavyojionesha nchini Nigeria ambako Kikundi cha Boko Haram kinataka kuwasilimisha wananchi wote wa Nigeria ili wawe ni waamini wa dini ya Kiislam, jambo ambalo linakwenda kinyume cha haki msingi za binadamu. Boko Haram ni tishio kwa maisha, usalama na ustawi watu: kiroho na kimwili.







All the contents on this site are copyrighted ©.