Hati elekezi kutoka kwa Mababa wa Sinodi kuhusu Familia
Mababa wa Sinodi baada ya kusali, kutafakari na kushirikishana: matatizo, changamoto
na fursa mbali mbali katika maisha ya kifamilia kwa muda wa juma zima, Kardinali Peter
Erdo, mwezeshaji mkuu, alitoa kwa muhtasari mambo msingi yaliyojadiliwa na Mababa
wa Sinodi, hati elekezi katika majumuisho ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu
kuhusu familia iliyoanza kikao chake hapo tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba 2014.
Hati elekezi
inajikita katika mambo makuu matatu: kusikiliza kwa makini mintarafu hali za kijamii
na kitamaduni, katika mazingira ambamo familia zinaishi; kufanya upembuzi yakinifu
kuhusu mikakati ya shughuli za kichungaji inayopaswa kuchukuliwa pamoja na kumwangalia
Kristo na Injili ya Familia.
Sehemu ya Kwanza ya Hati Elekezi inabainisha kwamba,
kimsingi familia ni ukweli na tunu msingi; ni chemchemi ya furaha na kinzani; ni bandari
ya mahusiano thabiti lakini wakati mwingine, mahusiano haya yanaacha madonda makubwa
katika maisha ya watu. Familia ni shule ya ubinadamu, inayopaswa kusikilizwa kwa umakini
mkubwa kwa kuzingatia makando kando yake yanayojikita wakati mwingine katika ubinafsi
uliokithiri na upweke wa kutupwa!
Katika mazingira kama haya, Mama Kanisa anatumwa
kutoa neno la faraja, kwa kutambua kwamba, binadamu asili yake ni Mungu mwenyewe,
changamoto na mwaliko wa kuthamini na kuenzi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.
Waamini wahamasishwe kujisikia kuwa ni kiungo muhimu cha maisha na utume wa Kanisa
hata kwa wale ambao wakati mwingine wamejikuta wakielemewa na mapungufu yao ya kibinadamu.
Hapa waamini wanahimizwa kujitaabisha kuyafahamu kwa kina mafundisho ya Kanisa sanjari
na kukimbilia huruma ya Mungu.
Sehemu ya Pili ya Hati Elekezi kutoka kwa Mababa
wa Sinodi inamwangalia Kristo na Injili ya Familia mintarafu historia ya ukombozi
wa mwanadamu, kwa kuonesha uhusiano wa dhati kati ya mwanaume na mwanamke wanaoshiriki
kikamilifu katika mpango wa kazi ya uumbaji inayokamilika kwa kazi ya ukombozi iliyotekelezwa
na Kristo mwenyewe. Ikumbukwe kwamba, familia ni sehemu ya mpango wa Mungu tangu kuumbwa
kwa ulimwengu.
Mababa wa Sinodi wanawataka waamini kufanya upembuzi yakinifu
kwa kuangalia tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, madonda wanayokabiliana nayo
pamoja na hali ambazo zinakinzana kimsingi na mafundisho pamoja na Mapokeo ya Mama
Kanisa, ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano ndani ya Kanisa. Hapa kinachozungumziwa
na uchumba sugu, ndoa za serikali, wanandoa waliotalakiana na kuoa au kuolewa tena.
Mama Kanisa anawatambua watoto wake wanaoshiriki katika maisha na utume wake hata
kama si katika utimilifu wake. Anatambua na kuheshimu tunu msingi wanazohifadhi katika
maisha yao, licha ya mapungufu yao ya kibinadamu.
Mababa wa Sinodi wanakazia
ukweli, uzuri wa maisha ya familia na huruma ya Mungu; mambo ambayo yametolewa ushuhuda
na Mababa wa Sinodi wakati wa maadhimisho; wanandoa wamekumbana na mawimbi mazito
katika maisha ya ndoa na familia, lakini bado wameendelea kushikamana na kupendana
kwa dhati. Ni wajibu na dhamana ya Mama Kanisa kuwasindikiza watoto wake ambao ni
dhaifu, kwa kuwajengea tena imani na matumaini ili waweze kukabiliana na changamoto
za maisha ya ndoa na familia.
Sehemu ya Tatu ya Hati Elekezi inagusia changamoto
na mikakati ya shughuli za kichungaji kama sehemu ya mchakato wa utangazaji wa Injili
ya Familia kwa Watu wa Mataifa. Mama Kanisa anatumwa kuwatangazia watu mbali mbali
katika mazingira yao tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kwa kutambua kwamba,
Uinjilishaji ni dhamana ya Watu wote wa Mungu na kwamba, watu lazima watangaziwe Injili
ya Familia na furaha inayoijaza mioyo ya watu.
Hapa kuna haja ya kujikita
katika wongofu wa kimissionari; lugha makini, majadiliano yanayosimikwa katika ukweli
na uwazi na kwamba Sakramenti ya Ndoa ni utume wenye: haki, dhamana na wajibu. Wanandoa
wapya wanapaswa kuandaliwa barabara ili waweze kufikia ukomavu wa kiimani, watambue
uzuri na changamoto katika maisha ya ndoa na familia, wafahamishwe kinzani zinazoweza
kujitokeza kutokana na masuala ya kiuchumi na kijamii. Waamini walei, wawasaidie wanandoa
katika kutekeleza dhamana na maisha yao ndani ya familia.
Mababa wa Sinodi
wanasema kwamba, Familia yote ya Mungu inawajibika kuwafunda wanandoa watarajiwa kwa
njia ya ushuhuda makini pamoja na kuwapatia mafundisho ya kina kwa kutambua kwamba,
kuna uhusiano mkubwa kati ya Sakramenti ya Ndoa na Sakramenti nyingine za Kanisa kama
chemchemi ya neema. Kabla ya kufunga ndoa, wanandoa watarajiwa washiriki kikamilifu
katika maisha na utume wa Kanisa na kwamba, wanandoa wapya wasindikizwe katika maisha
yao ya ndoa na familia katika miaka ya kwanza kwanza.
Mababa wa Sinodi wanasema,
Parokia ni mahali muafaka kwa wanandoa wapya kupata majiundo endelevu, kwa kuwahamasisha
kupokea na kulea zawadi ya maisha. Wasaidiwe kutambua tasaufi ya maisha ya ndoa na
familia, sala na matendo ya huruma. Wanandoa wapya wahamasishwe kushiriki katika Ibada
mbali mbali za Kanisa kwa kutambua kwamba, wao pia ni vyombo vya Uinjilishaji.
Mababa
wa Sinodi wameona cheche za mambo mema kwa "wachumba sugu", wasaidiwe ili hatimaye,
waweze kufikia maamuzi ya kufunga ndoa Kanisani. Ukosefu wa uhakika wa fursa za ajira,
mshahara wa kutosha kukidhi mahitaji ya familia ni kati ya mambo yanayopelekea watu
wengi kuendelea kuwa katika "uchumba sugu". Watu hawa wasaidiwe kuona na kutambua
tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, utume unaopaswa kutekelezwa kwa unyenyekevu
na uvumilivu mkubwa, hapa familia za Kikristo zinapaswa kuonesha ushuhuda kama vyombo
makini vya Uinjilishaji.
Mababa wa Sinodi kwa moyo wa upendo na mshikamano,
wanawaalika viongozi wa Kanisa kuibua mbinu mkakati mpya wa shughuli za kichungaji
kwa ajili ya wanandoa waliotalikiana na kuamua kuoa au kuolewa tena; familia ambazo
zinakumbana na madonda makubwa katika maisha na utume wake. Matatizo ya kiuchumi,
kijamii na kiimani, ni changamoto kwa Makanisa mahalia kuendeleza majadiliano ya kina,
ili kujenga na kuimarisha uaminifu kwa Injili ya Familia. Waamini hawa wahudumiwe
kwa huruma na mapendo. Wasikilizwe kwa umakini, wapendwe na kuthaminiwa. Bado kuna
changamoto kubwa katika ndoa mseto.
Mababa wa Sinodi wanasema, Kanisa ni nyumba
inayopaswa kuwakaribisha wote hata wale wanaoishi katika ndoa za watu wa jinsia moja,
bila ya kuhatarisha wala kubeza mafundisho tanzu ya Kanisa Katoliki kuhusu ndoa na
familia. Hii ni changamoto kubwa katika malezi na majiundo ya waamini. Kanisa halitakubali
kushinikizwa na Mashirika ya Kitaifa na Kimataifa ka kisingizio cha usawa wa kijinsia.
Waamini watambue matatizo na changamoto za kimaadili zilizoko mbele yao. Haki msingi
za watoto zinapaswa kuzingatiwa na walezi wa jinsia moja.
Mababa wa Sinodi
wanawahimiza wanandoa kupenda na kuthamini maisha kama kielelezo cha upendo wao. Wafundishwe
njia asilia za uzazi ili waweze kufurahia maisha yao ya ndoa, kwa kuheshimu na kuthamini
utu na heshima ya binadamu inayojikita katika Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa
kifo. Wanandoa waendelee kupatia majiundo endelevu.
Mababa wa Sinodi wanasema
kwamba, elimu na dhamana ya familia ni kati ya changamoto kubwa katika azma ya Uinjilishaji.
Familia zijitahidi kuonesha mfano bora wa kuigwa kwa kujenga mazingira bora ya makuzi,
urithishaji wa tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu na kwamba, Kanisa litaendelea
kuenzi familia katika utekelezaji wa dhamana na utume wake.
Mwishoni Mababa
wa Sinodi wanakiri kwamba, hati hii ni matunda ya mchango wa mawazo uliotolewa katika
misingi ya ukweli na uwazi; kwa kusikilizana na kuheshimiana na kwamba, tafakari hii
iendelee kufanyiwa kazi kwenye Makanisa mahalia, ili Maadhimisho ya Sinodi ya kawaida
ya Maaskofu itakayoanza hapo tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015 iweze kuzaa matunda
yatakayoliwezesha Kanisa kutangaza Injili ya Familia.
Imetayarishwa na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.