“Mnuso” ni utamu utokanao na kunusa harufu nzuri. Katika matumizi ya kiswahili cha
mitaani neno hilo linamaanisha sikukuu au sherehe, nk. Mathalani sherehe za ndoa wanaita
“Mnuso wa Arusi.”
Sifa ya kwanza ya mnuso wowote ule, ni kufurahi, kusherekea,
kushangilia kwa kula na kunywa hata kucheza. Sifa ya pili ya mnuso ni kusherekea bure,
yaani unaalikwa kufaidi bure, hakuna kudaiana michango wala kutoa zawadi. Unachotakiwa
kuingia nacho kwenye mnuso ni nja na kiu yako, sanasana uwe tayari na furaha ya kujichana.
Sifa ya tatu ya mnuso ni kupata fursa ya kusherekea pamoja na mwenye sikukuu, au na
mgeni rasmi.
Masuala ya minuso ya arusi yalianza zamani sana hata kabla ya
Yesu. Wakati wa Yesu watu walikuwa wanazungumza na kuotea ndoto juu ya mnuso wa bustani
ya Edeni. Kwa vile watu walikuwa katika mzingira ya kuteseka, watu wakawa wanaotea
ndoto ya kuwa na ulimwengu wa mnuso kama ule wa bustani ya Edeni, yaani ulimwengu
wa Padadisi, kwa ajili ya watu wema ambao wanateseka. Ndoto aina hiyo inasimuliwa
pia katika kitabu cha Nabii Isaya anaposema: “Bwana ataandaa karamu katika mlima Sion,
karamu ya divai tamu, chakula”. Kwamba Mungu mwenyewe ataandaa mnuso. Marabi waliendelea
kusema kwamba wakati huo utakapokuja, yaani mwisho wa dahari, watakatifu watakaa pamoja
na Mungu na kila mmoja atasema: “Tazama huyu ndiye Mungu wetu.”
Msingi wa mahubiri
ya Yesu ni kujenga ufalme wa Mungu, ambao katika injili ya leo tungeweza kuuita “Mnuso
wa arusi”. Yesu mara nyingi anaanza mahubiri yake kwa kutangaza: “Wakati umetimia,
na Ufalme wa Mungu umekaribia” (Mk 1:15) toka hapo najiegemeza kwenye mifano mbalimbali
anayotoa na ndivyo polepole anafunua “fumbo” la huo ufalme anaotaka kuujenga ulimwenguni.
Katika
mandhali kama hii ya kitamaduni na ya kutaka kujenga “Ufalme wa Mungu” Yesu anatuletea
mfano huu wa leo, wa baba mtu (mfalme) anayeandaa mnuso wa arusi kwa ajili ya mtoto
wake. Yesu anaanza kusema: “Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyemfanyia
mwanae arusi.” Hapa Yesu anataka kuzungumzia juu ya karamu au sherehe za hapahapa
duniani, tofauti na karamu waliyomaanisha marabi yaani ile ya Eden au paradisi ya
ulimwengu ujao baada ya kifo.
Kumbe, Mungu anataka watoto wake waishi kwa
furaha hapa duniani katika mazingira ya sikukuu, ya sherehe za ndoa, mazingira ya
furaha na ya upendo. Unapoutazama ulimwengu wa leo, huwezi kuiona picha hii ya paradisi
ya Eden ya karamu na ya sherehe, yaani karamu ya mahusiano mapya, ya furaha ya sherehe
ambayo yanawakilishwa na karamu ya ekaristi takatifu. Kwa vyovyote hatuwezi kusema
kuwa ulimwengu huu ni wa watu wanaosherehekea arusi kama tusikiavyo katika injili
ya leo, badala yake tunaona na kusikia juu ya vita kila mahali, tunaona watu waliokata
tamaa, wakimbizi, madhulumu, kukandamizana, nk.
Kumbe ukweli wa mambo, ulimwengu
huu ni bustani ya paradisi ambayo Mungu ameiandaa, nasi binadamu wote tumealikwa kuingia
kuifaidi. Kinyume chake tunawaona waalikwa wachache ndiyo wanaofaidi mnuso, kwa sababu
wamejibinafsisha ulimwengu huu, wamewatenga waalikwa wenzao na mbaya zaidi wamemsahau
hata mwandaaji wa mnuso huu.
Mtayarishaji wa mnuso wa arusi katika mfano wa
leo ni Mungu mwenyewe. Yeye anataka wanawe waishi katika ulimwengu huu kama vile
wangekuwa arusini. Yaani kuishi kwa amani na upendo na kuufaidi pamoja ulimwengu huu.
Hapa ndipo linapoingia suala la endapo waalikwa wanakubali mwaliko wa kuja kuungana
pamoja, kujenga mahusiano ya kisherehe na ya furaha ya pamoja katika karamu hii ya
ufalme mpya inayowaunganisha watu wote, yaani kujenga mahusiano kati ya watu katika
ulimwengu huu. Kinyume na kuendeleza ulimwengu wa kale wa kuishi kila mmoja kivyake
na kibinafsi. Yesu peke yake alitoa wazo hili la ulimwengu mpya wa mnuso wa arusi
ulio tofauti na ulimwengu wa kale. Katika ulimwengu huo wa kale waalikwa wengine hawajisikii
kwa sababu waalikwa wenzao wamejimilikisha na kuutamalaki ulimwengu wote. Wamemiliki
vyakula vyote, mamlaka yote, mali asili yote nk.
Hapa ndipo unapoona sababu
ya hali halisi ya kuwepo kwa vita na magomvi katika ulimwengu. Kutokana na vurugu
hizo, hali ya hewa ya karamu au sherehe inabadilika. Mnuso unageuka kuwa mnuko. Kumbe
karamu iliandaliwa ili kutosha wote endapo kungekuwa na ustaarabu, lakini bila utaratibu
chakula hakitatosha kwa wote kwani kimevamiwa na wachache wenye ubinafsi. Vurugu hilo
linafanywa na wale wanaochukua chakula bila kufuata utaratibu wa haki na upendo kadiri
ya malengo ya mwandaaji yaani Mungu.
Kwa hiyo, mfano huu unahusu mahusiano
ya walioalikwa kwenye kutumia mali ya ulimwengu huu kwa haki ili kutosha kwa wote,
ili wote wawe na furaha. Masilahi ya ulimwengu huu (sherehe hizi za arusi) ni mengi
na yametayarishwa ili kuwatoshea wote. Huu ndiyo ulimwengu mpya wa ufalme mpya wa
Mungu nasi sote tumealikwa kuuishi na kuufurahia.
Kuna makundi matatu ya watumwa
waliotumwa kutawanya mialiko. Makundi mawili ya mwanzoni yanatumwa kwa awamu. Watumwa
hawa ni manabii wa agano la kale. Bwana anasema: “Tazameni, nimeandaa karamu yangu;
ng’ombe zangu na vinono vimekwisha kuchinjwa, na vyote vimekuwa tayari, njoni arusini.
Lakini waalikwa hawakujali, wakaenda zao, mmoja shambani kwake, mwingine kwenye biashara
zake, na wengine waliwakamata watumwa wale wakawatenda jeuri hata kuwaua.”
Watumwa
hawa wanadhulumiwa na kuuawa kwa sababu katika ulimwengu wa kale, wale waliokuwa na
mashamba makubwa na mapana na shughuli na miradi yao, walikuwa na nguvu, na uwezo
na walikuwa matajiri. Hao hawakuwa na haja ya kwenda kwenye minuso, kwani walisharidhika
na maisha yao. Hivi hawakutaka hata kuingia katika ulimwengu mpya bali wakaamua kubaki
katika ulimwengu wao wa kale, ulimwengu wa binafsi siyo wa kushirikiana mambo.
Kwa
hiyo, endapo watumwa waliwakera na kuwabugudhi mno, wakawafukuzilia mbali, na wakati
mwingine waliweza hata kuwaua. Hivyo ndivyo walivyofanyiwa manabii wa kale. Watu
hao walielewa vizuri sana mwito huo wa kuingia arusini, uliowadai kuachana na ulimwengu
wa kale na kuingia katika ulimwengu mpya wa haki na upendo. Yaani ulimwengu wa kusherekea
mnuso pamoja.
Kabla ya sehemu ya pili ya mfano, yaani ya kuingia kundi la watumwa
kwenda kutawanya kadi za mwaliko kwa awamu ya tatu, kimeingizwa kituko kimoja kinachovuruga
mfululizo mzuri wa mfano. Kipengee hicho chasema hivi: “Basi yule mfalme akaghadhibika;
akapeleka majeshi yake, akawaangamiza wauaji wale, akauteketeza mji wao. Kisha kawaambia
watumwa wake, arusi i tayari lakini walioalikwa hawakustahili.” Sehemu hii inasimama
peke yake na ina maana ya peke yake. Sehemu hiyo ni somo la kitaalilimungu juu ya
kile kilichotokea Yerusalemu. Mji wa Yesusalemu unawakilishaa mapato ya kukataa mapendekezo
na mwaliko wa kushiriki mnuso wa ufalme wa Mungu, yaani kushiriki karamu, wa kuacha
udhulumu.
Kutokana na kukataa huko hata Yesu akasema halitasalia jiwe juu
ya jiwe. Ndipo sehemu hiyo ikaingizwa, kama vile ungekuwa adhabu, au laana kutokana
na kumkataa Kristu. Lugha hii kali inaakisi lugha ya Agano la kale, ambako makosa,
dhambi inaoneshwa kuwa itakuja kuadhibiwa vikali na Mungu, kumbe ukweli wa mambo Mungu
haadhibu, bali hayo ni mapato ya dhambi kwa mtu mwenyewe anayeitenda. Pale tunapomkataa
Kristu tunajiadhibu wenyewe. Hayo ndiyo mapato ya dhambi.
Kwa namna hiyo,
tunaweza kutafakari ulimwengu wa leo na matukio yake juu ya dhambi. Ujumbe muhimu
ni kwamba, yule anayekataa mapendekezo ya Kristu, mapato yake unayaona jinsi limwengu
unavyoenda. Madhulumu, vita, maangamizi, uonevu, kutoelewana, magomvi katika famili,
mashindano nk.
Baada ya kituko hicho cha mji wa Yerusalemu, sasa tukione kikundi
cha tatu ambacho mfalme anakiagiza tena: “Basi enendeni hata njia panda za barabara,
na wote mwaonao waiteni arusini.” watumwa hawa wa kundi la tatu ndiyo mitume na sisi
pia. Hao ni watumishi wapya wa Agano Jipya. Watumishi hawa wanaenda kuwaalika watu
wote wema na wabaya, vilema, maskini, na wapita njia, watu wenye shughuli zao, yaani
wapagani.
Hapo kunakuwa na timbwili la watu wa kila aina. Tungetegemea sasa
lango la jumba la sherehe lingefungwa na sherehe zianze. Ndivyo itakavyokuwa katika
ulimwengu ujao ambao walioingia paradisini watakuwa wameshaingia, milango itafungwa
na mnuso unachukua kasi yake. Kumbe hii ni sherehe au paradisi ya hapa duniani, milango
haifungwi, mapato yake kunatokea kasheshe nyingine mle jengoni.
Hebu fuatilia
jinsi ilivyokuwa. Mfalme akaingia na kuwakagua walioalikwa. Kisha akamwona mwalikwa
mmoja asiye na vazi la arusi akaanza kumwandama. Akaamrisha wamfunge na kumtupa nje.
Kulikoni, kwani yeye alikuwa kati ya waalikwa wa mitaani, na waliokuwa katika misafara
yao wasingeweza kujiweka sawa kabla. Halafu mbaya zaidi, humo walialikwa watu wa kila
aina na wenye mivao tofauti tofauti lakini sasa anaadhibiwa mtu kutokana na kutokuvaa
vazi la arusi tu.
Ndugu zangu sehemu hii imekaa safi tu. Kwanza sehemu hii
haina muunganiko na sehemu iliyopita, imekaa peke yake na ni mfano wa peke yake ulioletwa
ili kutoa tafsiri hii, kwamba unaweza kuingia kwenye karamu lakini unazo bado fikra
za kale, na ya vigezo vya kale, hilo ndilo vazi la kale na siyo sare ya mnuso mpya
wa arusi. Yawezekana kuwa wewe ukajisikia uko ndani ya mnuso, ndani ya kanisa, lakini
kumbe ukweli unaendelea kufikiri na kuishi kama wale walio nje.
Hivi uwepo
wako mle ndani ni wa nje tu. Lugha hii ni kwa ajili ya kumwonya mhaini, iwe wa dini
au wa chama au serikali, mtu anayejifanya yuko ndani kumbe fikra zake ziko nje. Ndiyo
maana Yesu anahitimisha “Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache.” Wote
wamealikwa, tena wako wengi wanaoingia katika chumba cha arusi, lakini ni nani hasa
ameitwa au ameelewa na amepokewa katika mnuso wa arusi mpya aliyoiandaa Mungu kwa
ajili ya mwana wake Yesu Kristu na ulimwengu mpya.