2014-10-13 16:01:36

Papa: Wema wa Mungu hauna mipaka, wala ubaguzi


(Vatican Radio) Baba Mtakatifu Francisko , Jumapili akihutubia mahujaji na wageni wakati wa sala ya Malaika wa Bwana alisema, "wema wa Mungu," haujui mipaka wala kubagua dhidi ya mtu yeyote, kila mtu anapewa nafasi ya kuitikia mwaliko wake, wito wake na kumwamini..

Hotuba ya Papa ililenga katika somo la Injili la Jumapili, kutoka Injili ya Matayo, ambamo mna mfano wa Mfalme anayetoa mwaliko wa Sikukuu ya harusi, ambamo waalikwa hawakuhudhuria na hivyo mwaliko unatolewa kwa wote, baadhi wanakubali na wengine kukataliwa.

Aliendelea kusema kwamba "hakuna hata mmoja kati ya wale waliochaguliwa kwanza, waliokubali kushiriki katika sikukuu hii. Kila mmoja alikataa kwa sababu zake, kwamba tayari alikuwa na mpango mwingine, na wengine walionekana kutojali tu na hata kukerwa na mwaliko waliopewa. Papa aliendelea kueleza, licha ya mwaliko kukataliwa, Mfalme hakukata tamaa, wala kuifuta sherehe , badala yake alitoa mwaliko huo kwa watu wote hata nje ya mipaka yake yote , na kuwatuma watumishi wake waende katika mitaa yote na katika njia panda zote, kuwakusanya wote watakao patikana.

Papa Francisko kisha alifafanua kwamba huku ni kukataliwa kwa Injili na baadhi ya watu, na bila kutarajia Injili inahubiriwa kwa watu wote, wote wakipewa mwaliko wa kushiriki katika Ibada. Hivyo wema wa Mungu, unaonekana kutokuwa na mipaka na wala ubaguzi dhidi ya mtu yeyote, kila mtu anapewa nafasi ya kuitikia mwaliko huu.

Aliendelea hii ina maana kwamba, tunahitaji kufungua mioyo yetu kwa wote hata walio pembezoni mwa jamii, na kutambua kwamba, hata wale waliosahaulika pembezoni, au wale wanao dharauliwa na kukataliwa na jamii, mbele ya Bwana wote wanathamani kubwa kwa kuwa Bwana, Mungu wa Upendo na wote wameumbwa kwa ukarimu wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko baada ya sala ya Malaika wa Bwana, alielekeza mawazo yake kwa watu waliofikwa na maafa ya maporomoko ya aridhi huko Genoa, Kaskazini mwa Italia, akionyesha, kiroho, kuwa pamoja nao, katika mahangaiko na mateso ya wote walio athirika kwa maafa hayo hasa walio poteza makazi na mali pia.

Katika kujali hali ya watu hawa, siku ya Jumamosi, Papa Francisko, alifanya mazungumzo kwa njia ya simu na Askofu Mkuu wa Genoa, Kardinali Angleo Bagnasco, ambaye Ijumaa mara baada ya kupata taarifa za mafuriko, aliondoka na kuuacha Mkutano wa Sinodi, na kwenda kushirikiana na wenzake wakati huu wa mateso makubwa ya watu katika mji wa Genoa. Maafa haya yanaweza kuwa mabaya zaidi kutokana na mvua kubwa kuendelea kunyesha katika eneo hilo la Kaskazini mwa Italia. Na imesikitisha zaidi kwamba, mafuriko haya yametokea wakati watu wako katika hatua za kujiinua baada ya kukumbwa na maafa kama haya miaka mitatu iliyopita. Hivyo juhudi zao zimerudisha nyuma.

Aidha Papa Francisko wakati huo wa Sala ya Malaika wa Bwana, alilikumbuka tukio la kutangazwa kuwa Mwenyeheri, Mtumishi wa Mungu Padre Francesco Zirano, aliyeuawa kikatili kwa kukataa kukana imani yake na badala yake aliongeza uaminifu wake kwa Kristo. Papa amemtaja kuwa ni mfano mzuri wa kuigwa na wafuasi wote wa Kristo, hasa katika mazingira ya mateso makali yanayotokana na kuwa Mkristo.
Mwenye Heri mpya Padre Francesco Zirano, ametajwa kuwa shujaa wa Injili.









All the contents on this site are copyrighted ©.