2014-10-13 10:47:23

Jengeni vituo vya afya, kila kata!


Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amewataka viongozi wa mkoa wa Tabora wajipange vizuri na kuhakikisha kuwa wanajenga vituo vya afya katika kila kata za wilaya ya Urambo kwa sababu bado iko nyuma.
“Hatua hii itasaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye hospitali ya wilaya ya Urambo kwa sababu yenyewe imekuwa ndiyo kimbilio la kila mgonjwa kwa sasa,” amesema.
Ametoa agizo hilo Jumapili, Oktoba 12, 2014, wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa mji wa Urambo mara baada ya kuzindua jengo la Mama Ngojea linaloitwa Mayu Lindila lililopo kwenye hospitali ya wilaya hiyo.
“Wilaya yenu ina kata 16, ina vijiji 57 na zahanati 22 lakini ina kituo kimoja tu cha afya. Na hii maana yake ni kwamba kuna vijiji havina zahanati kabisa. Huu ni mtihani mkubwa na ndiyo maana kila mtu akiumwa anakimbilia kwenye hospitali ya wilaya,” alisema Waziri Mkuu.
“Kisera kila kata ni lazima iwe na kituo cha afya, kwa hiyo viongozi wa mkoa na wilaya ni lazima mjipange kuona ni kwa namna gani mtaitekeleza sera hii, na pia jengeni zahanati kwenye vijiji ambavyo havina zahanati,” alisisitiza.
Akizungumzia kuhusu umuhimu wa huduma ya Mama Ngojea, Waziri Mkuu alisema unasaidia kuokoa maisha ya mama mjamzito anayetoka kata ya mbali ambaye anakabiliwa na tishio lakini siku zake za kujifungua zinakuwa hazijafika.
Alisema kutokuwepo kwa majengo ya Mama Ngojea katika maeneo mengi ni changamoto kubwa na hatari kwa akinamama wengi hasa waishio mbali na huduma za tiba. “Hivi kama kata moja iko mbali na makao makuu ya wilaya, na mama mjamzito mwenye tatizo hawezi kufika hospitali unadhani ataenda wapi? Si ataenda kwa wakunga wa jadi au waganga wa kienyeji tu?”
Aliwasihi akinamama wa wilaya hiyo wajitahidi kutumia huduma za hospitali kwa sababu kwa wakunga wa jadi na waganga wa kienyeji hakuna wataalamu kama waliopo hospitalini.
Alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Bibi Fatma Mwassa afanye utaratibu ili kila wilaya pawe na Mama Ngojea. “Hata kama hakuna hospitali ya wilaya lakini pana kituo cha afya, ni vema pawe na jengo la Mama Ngojea ili kuokoa maisha ya akinamama.
Akitoa taarifa ya ujenzi wa jengo hilo, Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Dk. Kheri Kagya alisema jengo hilo lenye uwezo wa kulaza wagonjwa 24 kwa wakati mmoja, lilianza kujengwa Agosti 25, 2012 na lilikamilika Novemba 10, 2013 kwa gharama ya sh. milioni 198/-. Lina jiko, sehemu ya kulia, mabafu, vyoo, eneo la kufulia na kupumzikia.
Lengo la kujenga kituo hiki ni kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 228 kwa kila vizazi hai 100,000 na kufikia vifo 90 kwa kila vizazi hai 100,000 au chini ya hapo ifikapo mwaka 2015. “Mwaka 2012 tulikuwa na vifo 253 kwa kila vizazi hai 100,000 na mwaka jana tulikuwa na vifo 228 kwa kila vizazi hai 100,000. Nia yetu ni kupunguza kabisa vifo vya akinamama kabla na wakati wa kujifungua,” alisema.
Aliwashukuru Mbunge wa jimbo la Urambo ambaye pia ni Waziri wa Afrika Mashariki, Bw. Samuel Sitta na mkewe Mama Margareth Sitta (ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa huo) kwa kubuni wazo hilo na kutafuta fedha za kujenga Mama Ngojea kwenye hospitali ya wilaya hiyo.
Wakati huohuo, Bwana na Bibi Sitta wamechangia mablanketi 300 na vyandarua 100 kwa ajili ya Mama Ngojea pamoja na hospitali ya wilaya hiyo.








All the contents on this site are copyrighted ©.