Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amewataka viongozi wa mkoa wa Tabora wajipange
vizuri na kuhakikisha kuwa wanajenga vituo vya afya katika kila kata za wilaya ya
Urambo kwa sababu bado iko nyuma. “Hatua hii itasaidia kupunguza msongamano wa
wagonjwa kwenye hospitali ya wilaya ya Urambo kwa sababu yenyewe imekuwa ndiyo kimbilio
la kila mgonjwa kwa sasa,” amesema. Ametoa agizo hilo Jumapili, Oktoba 12, 2014,
wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa mji wa Urambo mara baada ya kuzindua jengo
la Mama Ngojea linaloitwa Mayu Lindila lililopo kwenye hospitali ya wilaya hiyo. “Wilaya
yenu ina kata 16, ina vijiji 57 na zahanati 22 lakini ina kituo kimoja tu cha afya.
Na hii maana yake ni kwamba kuna vijiji havina zahanati kabisa. Huu ni mtihani mkubwa
na ndiyo maana kila mtu akiumwa anakimbilia kwenye hospitali ya wilaya,” alisema Waziri
Mkuu. “Kisera kila kata ni lazima iwe na kituo cha afya, kwa hiyo viongozi wa mkoa
na wilaya ni lazima mjipange kuona ni kwa namna gani mtaitekeleza sera hii, na pia
jengeni zahanati kwenye vijiji ambavyo havina zahanati,” alisisitiza. Akizungumzia
kuhusu umuhimu wa huduma ya Mama Ngojea, Waziri Mkuu alisema unasaidia kuokoa maisha
ya mama mjamzito anayetoka kata ya mbali ambaye anakabiliwa na tishio lakini siku
zake za kujifungua zinakuwa hazijafika. Alisema kutokuwepo kwa majengo ya Mama
Ngojea katika maeneo mengi ni changamoto kubwa na hatari kwa akinamama wengi hasa
waishio mbali na huduma za tiba. “Hivi kama kata moja iko mbali na makao makuu ya
wilaya, na mama mjamzito mwenye tatizo hawezi kufika hospitali unadhani ataenda wapi?
Si ataenda kwa wakunga wa jadi au waganga wa kienyeji tu?” Aliwasihi akinamama
wa wilaya hiyo wajitahidi kutumia huduma za hospitali kwa sababu kwa wakunga wa jadi
na waganga wa kienyeji hakuna wataalamu kama waliopo hospitalini. Alimtaka Mkuu
wa Mkoa wa Tabora, Bibi Fatma Mwassa afanye utaratibu ili kila wilaya pawe na Mama
Ngojea. “Hata kama hakuna hospitali ya wilaya lakini pana kituo cha afya, ni vema
pawe na jengo la Mama Ngojea ili kuokoa maisha ya akinamama. Akitoa taarifa ya
ujenzi wa jengo hilo, Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Dk. Kheri Kagya alisema jengo hilo
lenye uwezo wa kulaza wagonjwa 24 kwa wakati mmoja, lilianza kujengwa Agosti 25, 2012
na lilikamilika Novemba 10, 2013 kwa gharama ya sh. milioni 198/-. Lina jiko, sehemu
ya kulia, mabafu, vyoo, eneo la kufulia na kupumzikia. Lengo la kujenga kituo hiki
ni kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 228 kwa kila vizazi hai 100,000
na kufikia vifo 90 kwa kila vizazi hai 100,000 au chini ya hapo ifikapo mwaka 2015.
“Mwaka 2012 tulikuwa na vifo 253 kwa kila vizazi hai 100,000 na mwaka jana tulikuwa
na vifo 228 kwa kila vizazi hai 100,000. Nia yetu ni kupunguza kabisa vifo vya akinamama
kabla na wakati wa kujifungua,” alisema. Aliwashukuru Mbunge wa jimbo la Urambo
ambaye pia ni Waziri wa Afrika Mashariki, Bw. Samuel Sitta na mkewe Mama Margareth
Sitta (ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa huo) kwa kubuni wazo hilo na kutafuta
fedha za kujenga Mama Ngojea kwenye hospitali ya wilaya hiyo. Wakati huohuo, Bwana
na Bibi Sitta wamechangia mablanketi 300 na vyandarua 100 kwa ajili ya Mama Ngojea
pamoja na hospitali ya wilaya hiyo.