Tuzitazame fadhila za hekima na busara katika maisha yetu .
Mpendwa wa kipindi cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo. Tuhitimishe makala
yetu juu ya fadhila za hekima na busara. Lengo letu: tunataka tujiunde hivi ili hekima
yetu, ujuzi wetu wa mambo, elimu yetu, idhihirike katika namna yetu ya kuishi. Hekima
ni nyenzo ya maisha bora, hekima ni lulu kuu kupita zote.
Ndiyo maana mfalme
Sulemani alipoambiwa na Mungu aombe chochote, hakuomba kingine isipokuwa hekima. Hekima
kama elimu ya mambo katika uhalisia wake, ndio dira ya kuongoza maisha yetu. Hata
kama tungekuwa na utajiri wa mali, tukikosa hekima katika kuitumia, basi mali hiyo
inageuka kuwa sumu ya kutuangamiza sisi wenyewe na kuwahatarisha wengine. Ndio maana
si mara chache tunaaswa, kwamba urithi mzuri kwa waana ni hekima/elimu.
Na
tuzitazame fadhila za hekima na busara katika maisha yetu ya kila siku. Sote katika
maisha tunaalikwa kuitafuta hekima. Na hekima hiyo yenye kutupatia sisi uhuru na usalama,
si nyingine bali ni hekima ya kimungu. Neno la Mungu linasema “Hekima huwatukuza wanawe
na kuwasaidia wale wanaomfuata. Ampendaye hekima anapenda maisha, wamtafutao hekima
mapema watajazwa furaha...Bwana awapenda wale wapendao hekima” YbS. 4:11-14.
Hekima
hiyo ya kimungu, itusaidie sasa katika maisha yetu. Itusaidie kuishi vema sisi wenyewe
na kuishi vema na jumuiya ya watu popote. Neno latuambia “ ifanye jumuiya ya watu
ipendezwe nawe” (YbS. 4:7. Ni kwa hekima na busara tu ndiyo twaweza kuwa wapendevu
mbele za watu. Hekima inatupatia nini cha kusema. Busara inatuelekeza ni wapi tuseme,
lini tuseme na kwa nani tuseme na nama gani tuseme. Tunaambiwa “usiache kusema wakati
unaofaa, wala usiifiche hekima yako” YbS 4:23.
Mintarafu mazungumzo, busara
ya maisha inatuelekeza hivi, kila mtu anapaswa kusema ukweli, lakini sio kila ukweli
unasemwa kwa kila mtu, na tena sio kila ukweli unasemwa kila mahali, na tena, sio
kila ukweli unasemwa na kila mtu, na tena sio kila ukweli unaoujua lazima uusema,
na zaidi sana sio kila jambo linalokusibu lazima ulitangaze kwa watu. Tunaambiwa “usimfungulie
kila mtu yaliyomo moyoni mwako” (YbS 8:19). Jilinde, Yoshua Bin Sira anasema “tunza
siri zako na uwe mwangalifu, maana unatembea kwenye hatari” 13:13.
Hapa kinachodaiwa
zaidi ni busara katika matumizi ya mdomo wako. Busara hiyo itakulinda. Mintaraufu
kusema sema, neno la Mungu linatuasa “usipepete nafaka kwa kila upepo...uwe mwepesi
kusikiliza lakini uwe mwangalifu katika kutoa jibu” YbS 5:9-11. Ndipo hapo tunaambiwa,
sio kila swali binafsi unaloulizwa lazima ulijibu. Kama wewe sio msemaji mkuu wa jambo
unaloulizwa, ni aheri kukaa kimya, sija baadaye ukashindwa kuyawajibikia maneno uliyoyasema.
Hekima
inatuambia ni vema kuwa na marafiki. Busara ituelekeze namna gani tuwapate marafiki
na namna gani tuishi nao. Tupo ambao tuna uzembe uliopitiliza, kila rafiki ajaye tunamwambia
siri zetu zoote. Kesho na kesho kutwa urafiki unapoingia dosari, basi moyo wako wote
unaanikwa mtaani. Tunahitaji kuwa na busara kubwa katika mahusiano, tuwe waangalifu
sana, hasa kwa hao unaowaita marafiki sako. Neno la Mungu linasema “ukitaka kupata
rafiki, mchunguze kwanza, usiharakishe kumwamini” YbS 6:5-17. Sasa tupo wenye bahati
mbaya ambao, unamfahamu mtu kwa siku mmoja tu, na siku hiyohiyo anakuwa rafikia yako,
na unamweleza siri zako na mipango yote. Kufanya hivyo ni kuiweka heshima yako hatarini.
Hekima
inatupatia jambo la kutenda. Busara inatuelekeza, wapi tutende, lini tutende na katika
mazingira gani tutende. Uzembe katika matendo daima umewafedhehesha wakuu. Kuna wakati
tumejisingizia kuwa sisi ni binadamu na hivyo tuna lazima ya kuwa wawazi. Ikumbukwe
kwamba ubinadamu sio tiketi ya uhovyo. Tuwapo katika jamii adilifu ni lazima kabisa
kuheshimu matakwa ya aibu. Hatuwezi kujiachia tu katika matendo ya aina zote bila
kujali mazingira wala wakati. Kufanya hivyo ni kujiaibisha mwenyewe na kukwaza watu
pia.
Nyakati zetu hizi za utandawazi, tunadaiwa kujilinda zaidi. Hekima yetu
ituambie wazi kuwa tupo katika nyakati si salama sana kimaadili. Busara ituelekeze
namna ya kuenenda ili tusijizolee aibu isiyofutika maishani. Katika ulimwengu wetu
huu, kuna vitu vingi vizuri sana, lakini sio kila kitu kizuri kinafaa! Wapo watu wengi
wazuri sana, lakini sio kila watu wazuri ni wema mioyoni. Busara ituelekeze namna
sahihi ya kutumia vyombo vya mawasiliano kwa kulinda zaidi utu na heshima ya mwanadamu.
Kwa sababu ya kukosa hekima ya kimungu na busara stahiki, leo hii vyombo vya mawasiliano,
kama vile simu za mkononi, tv hata kamera vimekuwa ni vyombo vya kurarua utu na heshima
ya mtu.
Hapa tunasema tena kwamba, kwa busara yako, kamwe usitumie mtandao
ili kuuponda utu wa mtu kwa kumuanika katika ufaragha wake. Kila mtu ana haki ya faragha.
Ila maadili yatukumbushe kwamba, tunahitaji faragha adilifu. Lakini pia kwa busara,
ni wajibu wa kila mmoja kujilinda ili usinaswe na waliofilisika maarifa. Ndipo hapo
tunakumbushia wito wa kijiwekea miiko katika maisha. Uwe na mwiko wa mazingira, yaani
usipende kuwa kila mahali. Tena, uwe na mwiko wa mahusiano, yaani usipende kuwa rafiki
ya kila mtu, usipende kumkaribisha kila mtu katika faragha yako, utaanikwa mtaani
na haitafutika. Tena, uwe na mwiko wa vyakula na vinywaji. Kwa busara ukijiwekea makatazo
binafsi ya maisha, utajiokoa na majanga mengi sana.
Lakini hilo lawezekana
zaidi kwa msaada wa Mungu. Tunaambiwa “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee
akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako”
(). Na daima tusali na mzaburi tukisema “Ee Bwana, unijulishe njia zako, Unifundishe
mapito yako, Uniongoze katika kweli yako, Na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu
wa wokovu wangu. Zab. 25:4- 5.
Kutoka katika Studio za Radio Vatican ni mimi
Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.