TAFAKARI YA NENO LA MUNGU DOMINIKA YA 26 YA MWAKA A, 28SEPTEMBA
TAFAKARI YA NENO LA MUNGU DOMINIKA YA 26 YA MWAKA A, 28SEPTEMBA Karibuni mpendwa
tusali pamoja tukiongozwa na neno la Bwana likitualika kubadili maelekeo yetu mabaya
na kumrudia Bwana. Mwaliko huu tunaupata katika mahubiri ya nabii Ezekieli katika
somo la kwanza akisema wajibu wetu ni kuacha dhambi na kuanza maisha mapya, maisha
yaliyojaa heri na fanaka nyumbani mwa Bwana. Na anawaonya wale wema watakapoghairi
njia ya haki, anguko lao ni kubwa na watakufa katika anguko hilo.
Nabii Ezekieli
anatoa mafundisho haya wakati Waisraeli wako utumwani Babeli, wanateseka na kulalamika
wakisema, kwa sababu ya dhambi za mababu zetu tunateseka hapa ugenini. Kumbe nabii
Ezekieli anaibuka akiwaambia kuwa kila mmoja wao anawajibika katika makosa yake kwa
hivi suala la baba zao kutenda dhambi si la msingi, la msingi ni kuacha njia mbaya
na kumrudia Bwana. Nasi hivi hivi twaweza kubaki katika kulalamika juu ya makosa ya
wengine tukasahau wajibu wetu wa toba katika maisha yetu ya imani. Tunapaswa kukumbuka
kila siku juu ya wajibu wetu wa ubatizo na si juu ya dhambi za wengine.
Mtume
Paulo anaendelea kuwaasa Wafilipi kukaa katika pendo la Bwana yaani kukwepa ugomvi
na ushindani unaokuza ubinafsi na majivuno, badala yake wakue katika unyenyekevu na
mapendo ya jirani yanayomweka mwenzangu mbele yangu daima. Kwa kukuza mapendo tunafuata
mfano wa Kristu aliyekuwa yunamna ya Mungu lakini alijinyenyekeza na kujifanya hana
utukufu akatwaa namna ya mtumwa, akawa mwanadamu na mwisho ametii mpaka kufa mauti
ya msalaba. Matunda ya unyenyekevu wa Kristu ni kwamba Mungu alimwadhimisha mno na
sasa kila goti linapigwa mbele yake. Si goti tu linalopigwa mbele yake bali wokovu
wa ulimwengu. Mpendwa msikilizaji, Sisi leo hatuna budi kufuata kiuaminifu mfano huo
wa Kristu mkombozi na hasa tunapotangaza neno la Mungu, tunapotunza familia zetu,
tunapoimarisha vyama vya kitume na aina nyingine ya utume katika Kanisa na nchi kwa
ujumla. Hatutadaiwa mambo makubwa bali matendo yaliyojaa unyenyekevu.
Mwinjili
Mathayo anatufundisha umuhimu wa kutenda kwa moyo na si kwa maneno akitupatia mfano
wa watoto wawili wa baba mmoja. Mtoto mmoja anaambiwa na baba yake kwenda shambani
na anaitikia kwa nguvu kuwa anaenda na baadaye haendi. Mtoto wa pili anaambiwa nenda
shambani na anasema siendi, na baadaye anapiga moyo konde anatubu na anakwenda shambani.
Kati ya hawa yule wa pili anatenda kwa moyo wa toba anapiga hatua kurudi kwa baba
yake na hivi anatimiza mapenzi ya baba yake.
Mpendwa, kumbuka toba ni
ya maana katika maisha ya kikristu na hata katika maisha ya kawaida. Kijana huyu aliyetubu
anatudhihirishia uwepo wa nafasi katika nyumba ya Baba kwa ajili ya watenda dhambi
wanaotubu, na hivi kinyume chake ni kwamba wale wote wanaojisikia kiburi na wema yaani
wale wanaosema tunaenda shambani na baadaye hawaendi hawana nafasi katika nyumba ya
Bwana. Kwa ujumla Mungu anatutaka mabadiliko ya moyo yaliyo makamilifu (total conversion).
Anatutaka tushike imani ambayo ni tendaji na tambuzi kwa mapenzi ya Mungu. Imani ambayo
humwona Mungu aliye upendo na si mfanya biashara ambaye hucheza na faida. Imani ambayo
humwona Mungu ambaye mawazo yake ni ya juu kuliko mawazo ya kibinadamu.
Mpendwa,
ni wakati wetu kutafakari na kuona zaidi namna tutakavyoendesha maisha yetu ili yaambatane
na mapenzi ya Mungu.Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard
Tiganya Cpps