Papa amepeleka zawadi ya amani kwa taifa la Albania
Jumapili hii 21 Septemba 2014, Baba Mtakatifu Francisco, amefanya ziara ya Kitume
katika mji wa Tirana Albania, ambako ameongoza Ibada ya Misa katika uwanja wa Mtakatifu
MamaTereza.Katika homilia yake, amehimiza raia wa Albania kuwa na imani na matumaini,
kuifungua mioyo yao kwa Kristo, na katika kutimiza wajibu wao kwa Kanisa na maisha
ya kijamii.
Hii ilikuwa ni mara ya Pili kwa Albnania kutembelewa na Papa.
Ziara ya kwanza ilifanywa na Papa Yohane Paulo 11 hapo tarehe 25 April, 1993, ikiwa
imepita miaka miwili baada ya kuagushwa kwa utawala wa kidikteta na kikomunisti.
Wakati
wa Ibada katika homilia yake Papa Francisko, amekumbusha mateso makali waliyo yaishi
mashahidi wafia dini wa Albania, Wakatoliki, Waotodosi na Waislamu.
Na pia
aliangalisha katika ukweli halisi kwamba ,taifa la Albania bado ni changa, na hivyo
akahimiza pamoja na kutosahau uchungu walioupita miaka ya nyuma,pia ni muhimu kusonga
mbele na mabawa ya matumaini.
Na akitafakari masomo ya Jumapili hii, Papa
amekumbusha jinsi Yesu alivyounda jumuiya ya Mitume wake 12 na wengine 72 na kuwatuma
wawili wawili kutangaza Neno la Mungu. Papa ameziita Jumuiya hizi kuwa , jumuiya ya
kimisionari , Jumuiya iliyokuwa katika njia , ikijishughulisha na kazi za kutembelea
nyumba hadi nyumba kutangaza Injili, wakianza na salaam maalum na zawadi ya amani
“ amani katika nyumba hii”.
Na hiyo ndiyo ilikuwa nia kuu ya Ziara ya Papa
kwa taifa la Albania ni kufika na kuiambia kila kaya ya Albania “Amani katika nyumba
hii , na Amani katika kila moyo wa raia wa Albania”.
Papa alieleza, katika
moyo wa kazi za mitume 72 pia inaonyesha uzoefu wa kazi za kimisioanri kwa jumuiya
za Kikristo za nyakati zote. Bwana Mfufuka na aliye hai, hakuwatuma tu mitume 12,
lakini Kanisa lote , na kila mbatizwa kuifanya kazi hii ya kutangaza Injili kwa watu
wote.
Papa alirejea jinsi siku za nyuma, milango ya Albania ilivyokuwa imefungwa
na minyororo ya ukana dini na madhulumu, ambavyo viligandamiza uhuru wa kidini.Watu
waliokuwa na woga katika kuutangaza ukweli na uhuru, walifanya kila lililowezekana
kumzuia Mungu kuingia katika mioyo ya watu, walimweka Yesu nje ya mioyo ya watu,
na Kanisa katika historia ya nchi hiyo , licha ya kuwa kati ya nchi za mwanzo zilizo
pata bahati ya kupokea mwanga wa Injili.
Baba Mtakatifu aliendelea kuitazama
hali halisi ya Albania akisema, imekuwa ni nchi ya Wafia dini , yenye kuwa na madhulumu
makali dhidi ya Wakatoliki ,Waotodosi na Waislamu pia. Na hivyo Papa ametoa mwaliko
wa nguvu kwa Wakristo, Maaskofu , Mapadre , Watawa na waamini walei,wasikubali kuinamia
unyanyasaji na vitisho vya utawala mbovu. Papa amewataka wawe imara kama ulivyokuwa
imara ule ukuta wa Scutari , ambao ni alama ya Wakatoliki wafia dini katika eneo hilo
ambao walimwanga damu yao kama wana kondoo na kuchipuka kama ua la sala.
Papa
amewatia moyo Waalbani akwamba, leo hii milango ya Albania i wazi na inaendelea kukomaa
katika hatua mpya za utendaji wa kimisionari kwa watu wote wa Mungu.Na hivyo kila
mbatizwa anayo nafasi yake katika kazi na utume wa kuinjilisha, na utendaji wa jamii
kwa manufaa ya wote. Papa ametoa wito kwa kila mmoja kusikiliza wito wake na kuitikia
kwa moyo wa ukarimu, kwenda na kuitangaza Injili, kuwa shahidi wa upendo, na kuimarisha
urithi wa mshikamano kwa ajili ya kuboresha hali ya maisha yenye haki zaidi na udugu
kwa watu wote.
Papa Francisco kisha, alikigeukia kizazi kipya cha Vijana na
kuwataka wajilishe kwa Neno la Mungu na kutembea na Kristo mioyoni mwao , kwa kuwa
Neno lake la Injili huionyesha njia ya maisha. Aliwahakikishia kwamba,kuwa na Imani
kwa Yesu,ni kuchagua maisha ya furaha yanayong’arishwa kwa kukutana na Kristo na
kutoa maana ya maisha ya kila binadamu, awe mke au mme.
Baba Mtakatifu alihimiza
mahusiano katika kazi za kichungaji na mwendelezo wa tafiti kwa ajili ya kuhamasisha
mabadiliko mapya chanya katika Kanisa na jamii nzima. Na kwa namna ya pekee amewahimiza
Vijana kutoogopa kutoa jibu kwa ukarimu kwa Kristo anayewaita kumfuata katika utumishi
wa Mungu na kwa jamii. Papa alimetolea sala zake ili kwamba watu wengi wanaume na
wanawake waweze kuusikia wito huu katika mwanga wa Injili na neema za Sakramenti.
Nyakati
za adhuhuri, baada ya Ibada ya Misa,Papa aliongoza sala ya Malaika wa Bwana. Papa
katika hotuba yake, alirudia kutoa ujumbe kwa vijana,ambamo aliwataka watafute msaada
wa maisha kwa Yesu Kristo. Alikumbusha anayejijenga kwa Krsito anajijenga katika
mwamba imara. Yesu mwenye kutufahamu vyema pale tunapokosea,hatuhukumu lakini husema,
“nenda sasa na usifanye dhambi tena(Gv 8,11). Kwa nguvu ya Injili na mfano wa Wafia
dini, tunapata kuelewa kusema hapana kwa kishawishi cha fedha, Hapana kwa uhuru wenye
ubinafsi, hapana katika kuwa tegemezi na ghasia.Badala yake ni kusema ndiyo katika
utamaduni wa kukutana, na ndiyo katika uzuri wa kutenda wema, ndiyo katika kuwa na
furaha kuu ya kina ya moyo.Ni ndiyo katika kuwa aminifu hata katika vitu vidogo
vidogo.Na kwa namna hiyo , inawezekana kuijenga Albania iliyo bora zaidi na dunia
nzuri zaidi.
Papa alikamilisha hotuba yake kwa kumrejea Mama Yetu wa Shauri
jema wa Scutari,akiomba msaada wake kwa Kanisa la Albania na watu wote wa Albania
na hasa kwa ajili ya familia, watoto na wazee. “Mama Maria ,awaongoze katika njia
ya kutembea pamoja naMungu,kuelekea tumaini lisilofadhaisha”.