"Saidieni watu kugundua upya tunu za imani katika maisha yao ya kila siku" -Papa
Vatican Radio) Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa alikutana na kundi la Maaskofu kutoka
Jamhuri ya Kidemkrasia ya Congo ambao wamefika Roma kwa ajili ya hija yao ya Kitume
ya kila baada ya miaka mitano kutembelea Kiti Kitakaifu na Idara za Curia ya Roma,
"ad limina visit". Maaskofu wa DRC, waliianza ziara hii tarehe 11 na inakamilika tarehe
15 Septemba 2014.
Papa Francisko akikutana na Maaskofu hao, alionyesha kujali
watoto wa DR Congo kusajiriwa katika vikosi vya kijeshi na kutumiwa kama ngao ya
jeshi. ili kupambana na tatizo hilo Papa ameshauri Maaskofu Katoliki wa DRC, kuimarisha
kazi zao za kichungaji kwa vijana. Pia Alitoa wito kwao kufanya yote katika uwezo
wao, kukuza amani na kutokomeza biashara haramu ya silaha.
Papa Francisco,
aliendelea kusema, vijana wa DRC, wanahitaji kuwa karibu na Mungu ili waweze kuvishinda
vishawishi vingi vinavyotokana na hali halisi ya maisha yao, hasa kushindwa kukamilisha
masomo au kupata kazi . Hili ni ni jambo la kutisha aliendelea, kwa sababu linavutia
watoto na vijana hawa, kuingia katika ajira mbovu kama wanamgambo hasa wanapolazimika
kuua vijana wenzao, katika ghasia za mapigano kiholela.
Na alinukuu waraka
wake wa Furaha ya Injili "Evangelii gaudium"akisema njia ya ufanisi zaidi katika
kushinda vurugu na ukosefu wa usawa na mgawanyiko wa kikabila n.k ni njia ya elimu
yenye kufundsisha mtu kufikiri kwa makini umuhimu wa kile anachotaka kufanya, na kuhimiza
maendeleo yenye kujenga ukomavu wa maadili. Papa aliomba kila Askofu awe mtumishi
wa vijana katika Jimbo lake.
Aidha kwa njia hiyo hiyo, aliendelea, wakiwa
wanakabiliwa na tatizo la kuvunjika kwa familia nyingi, hasa kutokana na vita na umaskini,
ni muhimu ya kukuza na kuhimiza juhudi za maendeleo kwa wote kwa lengo la kuimarisha
familia."
Kipengere kingine muhimu kilicho sisitizwa na Papa , ni haja ya
kusaidia umma kugundua upya umuhimu wa imani katika maisha yao ya kila siku na utendaji
kwa manufaa ya wote. Kwa unyenyekevu alisema, "Nawasihi, nyote, fanyeni kazi bila
kuchoka kwa ajili ya uanzishwaji wa haki na amani ya kudumu, maridhiano kwa njia ya
mazungumzo na kwa kusaidia mchakato wa kupunguza biashara haramu ya silaha". Wakati
huo huo, Papa alionya Maaskofu kuepuka kuchukua majukumu ya taasisi za kisiasa.
Pia
aligeukia suala la Mshikamano, akilenga zaidi utoaji wa msaada kwa waliolemewa na
ugumu wa maisha, watu maskini wa vijiji wazee, wagonjwa na walemavu, mipango ya kanisa
ielekezwe kwao zaidi.