Kardinali Napier- umuhimu wa Sinodi ijayo juu ya familia
Kardinali Wilfrid Napier, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Durban Afrika Kusini, hivi karibuni
amekuwa Rome kuhudhuria vikao mbalimbali vya utendaji katika Idara za Curia. Katika
mahojiano na Padre Paul Samasumo wa Redio Vatican, alizungumzia zaidi Familia ya Kikristo,
ambayo itakuwa kiini cha majadiliano katika Sinodi maalum ya Maaskofu, itakayofanyika
hapa Vatican mwezi ujao, Oktoba 05-19 juu ya mada "Changamoto za Kichungaji kwa familia
katika mazingira ya Uinjilishaji".
Kardinali Napier alilenga zaidi katika
barua juu ya familia iliyotolewa mwezi Februari na Sekretariat ya maandalizi kwa
ajili ya Sinodi, ambamo Papa Franciko ametoa wito kwa Wakatoliki, kuomba kwa ajili
ya Sinodi hiyo. Papa ameutaja Mkutano huu wa Sinodi juu ya familia, kuwa ni muhimu
na unawahusu watu wote wa Mungu - Maaskofu, Mapadre, Watawa wanaume na wanawake, na
wote walio yaweka maisha yao katika uaminifu wa Kanisa duniani kote. Wote wanashiriki
katika juhudi hizi za maandalizi kwa ajili ya mkutano huu, kupitia mapendekezo ya
utendaji na msaada muhimu wa sala.
Kardinali aliendelea kuirejea barua
hiyo ya Papa Francisco pia akionyesha matumaini yake kwamba, itakuwa kweli sinodi
maalum ambayo itafuatiwa na Mkutano wa Sinodi ya kawaida ya Maaskofu, mwaka ujao,
ambao pia madhari yakeni juu ya familia.