Papa aungana na Maaskofu kutoa wito wa amani Lesotho
Jumapili 7 septemba, baada ya sala ya Malaika wa Bwana, akizungumza na makumi elfu
ya mahujaji na wageni, katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro Papa Francisko,
alitoa wito wa amani kwa mataifa mawili, Lesotho na Ukraine.
Akizungumzia
Lesotho, Papa Francisco alisema pia anaongeza sauti yake katika wito wa Maaskofu
wa Lesotho, kuomba amani kwa taifa la Lesotho, ana alikemea vitendo vyote vya unyanyasaji
na kumwomba Bwana wa amani, arejeshe utulivu katika Ufalme wa Lesotho, amani ambayo
ni mizizi wa haki na udugu.
Siku ya Alhamisi, Gazeti la Lesotho Times, lilitaarifu
kwamba Baraza la Maaskofu Katoliki Lesotho (LCBC) lilitoa wito wa amani katika mazungumzo
kati ya vyama vya upinzani na utawala na pia walitoa wito kwa jumuiya ya kimataifa,
ihakikishe utulivu katika ufalme huu ambao kuna wasiwasi wa kufumka ghasia. Wito
wa Maaskofu ulitolewa kupitia mkutano wa vyombo vya habari katika mji mkuu, Maseru,
Lesotho na Askofu Augustinus Tumaole Bane, Askofu wa Leribe, kwa niaba ya Baraza
la Maaskofu, kwa vyama vya kisiasa na taasisi za kiserikali kama vile vyombo vya
usalama, kutatua tofauti zao bila ya kutumia vurugu. Na alisistiza haja ya kuwa
na uvumilivu katika utendaji wao. Katika mkutano wa vyombo vya habari, Askofu Bane,
alitoa wito huo akiwa na Maaskofu wenzake Askofu Joseph Mopeli Sephamola, Askofu Mkuu
Tlali Gerard Lerotholi, Askofu Mkuu Emeritus Bernard Mohlalisi, Askofu Emeritus Sebastian
Khoarai, na Askofu John Tlhomola.
Lesotho ni taifa dogo ambalo bado linaheshimu
mfumo wa utawala wa kifalme, lina raia milioni 2, na limezungukwa na Afrika Kusini.
Lilipewa uhuru kutoka ukoloni wa Uingereza mwaka 1966.
Matatizo ya hivi karibuni
Lesotho yalianza, Jumamosi tarehe 30 Agosti, wakati Waziri Mkuu Thomas Thabane alipotoroka
na kuvuka mpaka kuingia Afrika Kusini akisema alihofia maisha yake.
Na taarifa
za mapema Jumamosi wiki iliyopita zinaeleza, Jeshi la Lesotho , liliteka nyara kituo
Kikuu cha Polisi cha ufalme, na kufunga mawasiliano yote ya vituo vya Redio na simu.
Na milio kadhaa ya bunduki ilisikika tokea eneo hilo,ghasia zilizosababisha mtu mmoja
kupoteza maisha. Katika taarifa iliyotolewa na AFP jeshi limekanusha kuwa na mpango
wa mapinduzi ya kijeshi. Na kusisitiza kwamba walio vamia kituo kikuu cha Polisi
ni raia mashabiki wa kisiasa waliopata silaha kinyemela.
Waziri Mkuu wa Lesotho
Thomas Thabane alirudi Maseru, Ijumaa iliyopita, baada ya Rais wa Afrika Kusini Jacob
Zuma na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuingilia kati. Zuma ambaye
Mwenye kiti wa SADC, aliitisha mkutano wa dharura Pretoria. Baada ya mkutano kumalizika,
SADC ilimtaka Waziri Mkuu Thabane arudi Lesotho. SADC, iliahidi utendaji wa harakakurejesha
amani na utulivu Lesotho.
Baba Mtakatifu Francisko, wakati akitoa ombi lake
kwa taifa la Lesotho, pia wakati huohuo kukawa na habari mpya kwamba, mwanajeshi
Luteni Jenerali Tlali Kamoli, ambaye alikataa kuachia madaraka kama kamanda wa kijeshi
Lesotho, amechukua udhibiti wa ghala kuu la silaha, kwa hisia kwamba, pengine ni
maandalizi kwa ajili ya kuanzisha mapambano au hata vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Lakini tamko kutoka jeshi linaonyesha kuwa waminifu bado kwa Naibu Waziri
Mkuu, Mothetjoa Metsing, ambaye anayeongoza chama cha Lesotho Congress for Democracy
Party, ambaye ni mshirika katika Lesotho serikali ya mseto. Polisi inatuhumiwa kwamba
iko karibu sana na Waziri Mkuu Thabane, aliyejiondoa madarakani kwa kutoroka.
Papa
Francisko, anatumaini Serikali, wanasisasa na vyombo vya usalama, watasikiliza ombi
lake na lile lililotolewa na Maaskofu wa Lesotho, kudumisha amani na majadiliano
, kama tu njia inayofaa zaidi, kuondoa kasoro katika utawala, na kujenga haki katika
masuala halali na matarajio ya pande zote zinazohusika.