2014-08-29 09:50:51

Hatua zahitajika kulinda makundi madogo ya Wakristo Iraki


Jumuiya ya Umoja wa Mataifa kwa mara ingine, imehimizwa na uongozi wa Kanisa la Ulimwengu, kuharakisha utendaji thabiti utakaoweza kukomesha mara moja mateso na ukatili unaofanywa na Waislamu wasiovumilia wengine Kaskazini mwa Iraki. Wito huo ulirudiwa kutolewa siku ya Alhamisi, baada ya Baba Mtakatifu Francisko kukutana na Kardinali Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya kazi za Kichungaji kwa Wahamiaji na wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum. Majadiliano yao, yalilenga katika mahangaiko ya Wakristo wa Iraki na hatima ya vurugu na mauaji yanayoendeshwa na wapiganaji wababe wa Kiislamu wasiokuwa na uvumilivu kwa watu wasio Waislamu kwa lengo la kujadili hatma ya Wakristo wanaokimbia vurugu, mauaji na unyama unaofanywa na wapiganaji wa kiislamu wanajihad nchini Iraki.
Taarifa zinaonyesha maeneo mengi nchini Syria na Iraki, ambao kwa sasa yako chini ya udhibiti wa Kiisalamu, kuna kampeini za kigaidi, hasa dhidi ya makundi madogo ya watu wasiokuwa waislamu wakiwemo Wakristo.
Kardinali Vegliò akizungumza na Redio Vatican, baada ya kukutana na Papa, alisema kwamba, Papa amesema, Kanisa lazima liwe mstari wa mbele katika jitihada za kutetea wadhaifu, kwa kutoa msaada kwa wanaohitaji zaidi, maana haki zao zinagandamizwa. "Kanisa ni kwa ajili ya maskini na ni sauti ya wanaogandamizwa. Ni lazima lishiriki na kutochoka kutetea haki, kupitia mahubiri na hotuba; na kushawishi kama inawezekana, hali ya kisiasa. "
Kardinali vegliò aliendelea kusema kwa kurejea maneno ya Papa Francisko, aliyotoa wakati akirejea toka Korea, kwamba, ni halali kutafuta njia za kusitisha uchokozi na madhulumu. Lakini akasisitiza, umuhimu wa kutahimini kwanza njia inayofaa zaidi. Na kwamba ni juu ya jumuiya ya kimataifa kufanya tathmini hii, na kuonya hakuna kisingizio au udhuru kutofanya hivyo. Na kwamba, vinginevyo hatakuwa na tofauti na kile kilichofanywa wakati jeshi la Hitler lililofanya mauaji ya kinyama kwa Wayahudi, na baadaye wengi wakasema, hatukujua kama kulikuwa na unyama mbaya namna hiyo. Huo ni unafiki. Hivyo kwa wakati huu dunia imekwisha tangaziwa unyama unaofanyika Iraki na Syria, hakuna kiongozi wa taifa atakayeweza kusema hajui hilo. Hivyo ni wakati wa mshikamano wa Kimataifa kusitisha unyama huo sasa.
Kardinali Vegliò alieleza na kulaumu jumuiya ya Kimataifa, kwamba mpaka sasa imefanya juhudi kidogo mno, na hasa viongozi wa Umoja wa Mataifa na Ulaya, ambayo ni kijiografia wako karibu na kanda hii inayoteswa na vita.
Aliongeza, "Kwa bahati mbaya, Ulaya tuna matatizo mengi, na hasa kutokana na kumezwa na moyo wa ubinafsi na tunajifikiria na kujijali sisi wenyewe tu , na kupuuza yanayowatokea wengine. "Hata hivyo, matatizo yetu ni kidogo ikilinganishwa na yale yanayotokea Iraq, watu wanaokimbia ili kuepuka kuchinjwa kama mbuzi..”
Kardinali anatumaini Ulaya sasa itaonyesha kuguswa na madhulumu yanayofanyika na kuchukua hatua zinazostahili kukomesha unyama huo, kama baadhi ya nchi tayari zimeanza kufanya hivyo, walau kwa kuwapokea wakimbizi katika nchi yao kama Ujerumani, Ufaransa, Uingereza, Italia, Hispania, ambayo ni mataifa tajiri ikilinganishwa na wanakotoka wakimbizi. Na kwamba Kanisa pia limekuwa mshiriki katika kutoa jibu hili. Na aliweka bayana kwamba, inaposemwa Kanisa si tu kufikiria Vatican au idara "Curia", lakini ni juhudi za Kanisa zima kila mahali. Amesema Kanisa linaitikia vyema katika utoaji wa msaada kwa watu hawa maskini, wahamiaji na wakimbizi, waliokimbia makazi yao, kwa hofu ya maisha yao kukatizwa.








All the contents on this site are copyrighted ©.