2014-08-25 16:28:07

Hakika Kristu ni Mwana wa Mungu wa walio Hai, sote tukiri hivyo ....Papa


Kanisa ni watu wanaotembea na Mungu katika maisha yao ya kila siku wakiwa wamejawa na imani, upendo na matumaini kwa Mungu Baba. Ni jumuiya ya watu iliyoanzishwa na Yesu Mwana wa Mungu, ambayo hupata nguvu zake kutoka juu, na kuwa imara, mwamba wa imani isiyovunjika. Ni hotuba ya Baba Mtakatifu Francisko, siku ya Jumapili wakati wa sala ya Malaika wa Bwana, aliyosali pamoja na maelfu ya mahujaji na wageni, waliokusayika katika uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro.

Papa alieleza juu ya uhusiano wa waamini na Yesu kwamba, hujenga Kanisa. Na kwamba Yesu tangu mwanzo, alifikiri kuijenga jumuiya iliyo imara yaani Kanisa, mfano wa jengo imara. Na ndivyo alivyo mwita SimonI kati ya mitume wake kumi na wawili na kumpa jina jipya Petro, ambalo katika lugha ya kiebrania, lina maana ya mwamba. Katika Biblia neno hili mwamba, ni rejea kwa Mungu. Na SimonI alichaguliwa na Yesu, kuitwa Mwamba, (Petro) si kwamba alikuwa na sifa za kipekee za kibinadamu, lakini alikuwa na imani ya kweli thabiti kwa Yesu, imani iliyotoka juu.

Yesu alisikia moyoni mwake furaha kuu, kwa sababu alitambua Simoni, kwa neema ya Baba na Roho Mtakatifu, amepewa imani ya kumainika, ambamo, Yeye Yesu, ataweza kulijenga Kanisa lake, jumuiya ya waaamini wote wanaobatizwa katika Jina la Kristo. Yesu kwa upendo wake mkuu aliyatoa maisha yake kwa ajili ya Kanisa, watu waliosimikwa katika imani asilia thabiti , yenye kujenga uhusiano thabiti nae, uhusiano katika upendo, usharika na matumaini. Na haya ni mahusiano yanayopaswa kuwepo kati yetu sisi na Yesu kama Kanisa lake. Yesu anapenda kuliona kanisa lake alilo lianzishwa, linaendelea kutembea katika mwanga wa imani imara na matumaini thabiti katika njia yake.

Baba Mtakatifu alieleza na kusema , Ndugu zangu wapenzi, kile kilichotokea kwa Mtakatifu Petro , ni tukio na hoja kwa kila Mkristo, kuona ukomavu wake katika kumwamini Yesu Mwana wa Mungu aliye Hai . Na hivyo Somo la Injili ya Matayo 16;13-20, ni changmoto kwetu sote kujiuliza, kwa namna gani tunatembea katika njia hii ya imani kwa uaminifu? Kila mmoja analo jibu moyoni mwake. Baba Mtakatifu alieleza, Yesu anapenda kukaa katika moyo wenye imani ya kweli , aminifu na thabiti kama mwamba. Na yeye huyaona mawe yaliyo hai yanayo ijenga jumuiya yake , jumuiya iliyosimikwa kwa Kristo , jiwe kuu la pembeni.

Papa pia alizumgumzia upande wa Petro kwamba, kwa imani yake, alipewa dhamana ya kuwa mwamba wa Kanisa ambamo kanisa linajengwa juu yake, na hivyo kunatakiwa kuonekana umoja wa waamini wote kama kanisa moja lililojengwa juu ya mwamba huu, Petro. Somo hili ni mwaliko kwa kila mbatizwa, kutafakari msimamo wa imani yake , kwa sababu katika usharika wa imani, iwezekane leo hii kuendelea kujenga Kanisa lake moja Takatifu la Mitume, katika kila kona ya dunia, lililosimikwa katika mwamba imara.

Baba Mtakatifu alibaini kwamba , hata leo hii kuna watu wengi wanaofikiri kwamba Yesu alikuwa nabii mkuu na mwalimu wa hekima na mfano wa haki , lakini Yesu hata leo hii anawauliza wanafunzi wake, ambao ni sisi wabatizwa wote, je ninyi mwasema mimi ni nani? Papa alitoa mwaliko kwa wote kufikiri sana juu ya hilo. Kabla ya kutoa jibu, zaidi ya yote ni kumwomba Mungu Baba , kupitia kwa Mama Bikia Maria tupate neema ya zawadi ya kutoa jibu la kweli kutoka ndni ya mioyo yetu kukiri kwamba, Wewe ni Kristo , Mwana wa Mungu wa Walio Hai. Kuikiri imani kama tunavyosali katika sala ya kweli ya Nasadiki. Papa alikamilisha kwa kuwataka wote waliokuwa wakimsikiliza kurudia mara tatu maneno : Wewe ni Kristo , Mwana wa Mungu wa walio hai.








All the contents on this site are copyrighted ©.