2014-08-21 08:48:08

Uinjilishaji mijini!


Kardinali Lluis Martinez Sistach, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Barcellona, Hispania anasema kwamba, Waraka wa Injili ya Furaha, Evangelii gaudium uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko ni muhimu sana katika utekelezaji wa mchakato wa Uinjilishaji mpya na dhamana ya waamini walei kuyatakatifuza malimwengu. RealAudioMP3

Hapa Yesu Kristo anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza pamoja na kujenga mazingira yatakayowawezesha watu kukutana na Yesu, ili kumwinua tena mwanadamu aliyeanguka na kuelemewa na madhaifu yake. Umefika wakati wa kutangaza Injili ya Furaha kwa watu wa Mataifa, changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko. Miji inahitaji uwepo wa malaika wengi zaidi kuliko kujazwa na hofu za mashetani.

Mashetani wanaozungumzwa hapa ni ukosefu wa fursa za ajira, uchafuzi wa mazingira, umaskini wa hali na kipato, ukosefu wa makazi bora ya watu, mmong’onyoko wa tunu msingi za kimaadili na utu wema, watu kutoaminiana, ubinafsi, uchoyo, wizi na ufisadi, vita, nyanyaso, madhulumu na hofu!

Malaika wanaoendelea kuboresha maisha ya watu mijini ni pamoja na: familia, mahali ambapo watu katika raha na mahangaiko yao ya ndani wanapata kitulizo. Katika miji ile ambayo idadi ya Wakatoliki inazidi kupungua mwaka hadi mwaka, hapa ni kumwilisha Injili ya Furaha kadiri ya changamoto zinazotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, kwa kujikita katika ushuhuda wa maisha, kama chachu ya utakatifu, kiasi hata cha kujisadaka kama alivyofanya Askofu Oscar Romero. Wakristo katika miji mikubwa wanaweza kuwa ni malaika walinzi kwa kuendelea kusoma alama za nyakati.

Mikakati ya kichungaji katika miji mikubwa iwalenge na kuwashirikisha vijana ambao kwa sasa wengi wao wanaogelea katika mitandao ya kijamii, huko huko watangaziwe Injili ya Furaha na waelekezwe namna ya kukutana na Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Kanisa liendelee kujielekeza katika mchakato wa Uinjilishaji mpya kwa kujikita katika upendo, umoja na mshikamano wa kidugu unaoongozwa kanuni auni.

Waamini walei kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, wawe makini kueneza Injili ya Furaha kwa kuwashirikisha wengine ile furaha ya kukutana na Yesu. Licha ya kazi kubwa iliyofanywa na Mitume wa Yesu katika Kuinjilisha, lakini wanawake wa Kanisa la mwanzo kwa njia ya ushuhuda na tunu zao za kimama walikuwa mstari wa mbele katika mchakato wa Uinjilishaji, changamoto hata leo hii kwa Wanawake Wakatoliki kuhakikisha kuwa wanajifunga kibwebwe kuwaonjesha jirani zao ile furaha ya Injili, kwa njia ya ushuhuda na karama mbali mbali walizokirimiwa na Roho Mtakatifu.

Kanisa Katoliki katika miji mikuu liwe makini kusoma alama za nyakati anasema Kardinali Sistachi kwa kutambua fursa, matatizo na changamoto zilizopo, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Yesu Kristo ambaye ni chemchemi ya Uinjilishaji, kazi inayoendelezwa na Roho Mtakatifu.

Padre Jean Bosco Matand Bulembat, mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Kinshasa na bingwa wa Maandiko Matakatifu anasema, Yesu alikuwa na uhusiano mkubwa na miji ya nyakati zake alitembelea na kuhubiri: Nazareti, Capernaumu, lakini zaidi mjini Yerusalemu, kote huku Yesu alikuwa anamtafuta mwanadamu, ili kumwinua katika utu na heshima yake; kumwonjesha huruma na upendo wa Mungu bila ubaguzi. Kwa njia hii, Yesu alitambulikana na wengi kuwa ni Mwinjilishaji nambari moja!

Alionesha ujasiri na moyo wa kukutana na kila mtu, hii ndiyo changamoto kubwa inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko. Kanisa liwe na ujasiri wa kuwatangazia wafanyakazi na wakulima Injili ya Furaha, kwa kuwashirikisha wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Dhamana hii itekelezwe na waamini walei ambao kwa njia ya unabii, ukuhani na ufalme wao, wasaidie kuyachachua malimwengu kwa harufu ya utakatifu wa maisha.

Watu waonjeshwe upendo wa Mungu unaokoa na kuponya; watu watangaziwe Kweli za Kiinjili bila shuruti bali kwa kugusa katika uhuru wa mtu binafsi; waamini wawaonjeshe jirani zao upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake; washiriki katika raha na majonzi ya jirani zao.

Ikumbukwe kwamba, Kanisa lina dhamana ya Kuinjilisha, kumbe, Makleri wasikae wala kucheza mbali katika mcakato huu kwa umakini wa Neno la Mungu na ushuhuda wa maisha yao ya Kikuhani yenye mvuto na mashiko kwa watu! Kila siku kuna watu wapya wanaingia mijini, hawa wapokelewe na kushirikishwa maisha na utume wa Kanisa, hakuna mgeni wala “Mnyamahanga, Kyasaka wala mtu wa kuja”, wote ni wa Kristo!

Changamoto nyingine ni huruma na upendo wa kimama unaopaswa kuoneshwa na Kanisa, kwa kuwajali maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Ushuhuda na utakatifu wa maisha ni chachu ya Uinjilishaji mjini, watu wamechoka kusikia porojo, wanataka kuona imani katika matendo!

Imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.