2014-08-20 09:34:25

Inasikitisha kuona watu wanajitosa mhanga ili kusababisha vifo kwa wengine!


Askofu mkuu Alfred Adewale Martins wa Jimbo kuu la Lagos, Nigeria anasema kwamba, anasikitishwa na taarifa zinazotolewa kuonesha kwamba, Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram sasa kinaanza kuteka na kumiliki maeneo ya nchi, kiasi hata cha kulifanya Jeshi la Serikali ya Nigeria kuwa na wakati mgumu wa kuweza kuyakomboa tena maeneo haya yanayokaliwa na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram.

Askofu mkuu Martins anayasema haya kutokana na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram kuteka vijiji kadhaa Kaskazini mwa Nigeria na kuanza kuvitawala kwa mabavu pamoja na mfululizo wa milipuko ya mabomu ya kujitoa mhanga yanayoendelea kuhatarisha maisha na mali za wananchi wa Nigeria. Inasikitisha kuona kwamba, watu wanajitoa mhanga kwa kile wanachodhani kwamba, hii ni vita ya kidini.

Askofu mkuu Martins anaendelea kuwatia shime wananchi wa Nigeria kutokatishwa tamaa kutokana na mashambulizi yanayofanywa na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram pamoja na wasi wasi wa kuenea kwa mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, ambao kwa sasa unaendelea kuwa ni tishio la usalama na maisha ya watu Afrika Magharibi.

Hadi sasa Cameroon imefunga mipaka yake na nchi jirani kama sehemu ya mikakati inayopania kudhibiti kuenea kwa ugonjwa wa Ebola nchini humo. Cameroon imekuwa ikitoa hifadhi kwa makundi makubwa ya watu wanaokimbia mashambulizi ya kigaidi kutoka nchini Nigeria, kumbe kufungwa kwa mipaka ya Cameroon kuna madhara makubwa hata kwa wakimbizi kutoka Nigeria.







All the contents on this site are copyrighted ©.