2014-08-20 08:43:17

Epukeni kishawishi cha kuuza ubora wa elimu ili kupata kura za watanzania!


Shule Katoliki ni rasilimali ya thamani kubwa katika mchakato wa ujenzi wa upendo, umoja na mshikamano; ni mahali pa kurithisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni. Vijana warithishwe elimu inayosheheni: ukweli, wema, amani na upatanisho wa kijamii, ili vijana waweze kufahamu changamoto wanazokabiliana nazo katika hija yao ya maisha. RealAudioMP3

Askofu Severine Niwemuguzi, Makamu wa Rais Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kanisa Katoliki nchini Tanzania linajizatiti kuhakikisha kwamba, linatoa elimu bora ambayo kimsingi ina gharama zake. Hii ni changamoto kubwa kwa shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki kujikuta kwamba, zinatoza ada ya kiwango cha juu, kiasi cha kuwafanya watoto wa maskini kushindwa kupata elimu bora inayotolewa na Kanisa, ikizingatiwa kwamba, hawa ni walengwa wa kwanza.

Hadi sasa hakuna jibu la mkato kuhusiana na changamoto hii, lakini Familia ya Mungu nchini Tanzania inaendelea kutafakari jinsi ya kuziwezesha hata Familia maskini kupata fursa za elimu zinazotolewa na Kanisa.

Askofu Niwemugizi anasema kwamba, miongozo, sera na mifumo inayotolewa na Serikali ya Tanzania imekuwa ikiwachanganya wadau wa elimu hasa kuhusiana na viwango vya ufaulu wa mitihani ambao umegubikwa kwa kiasi kikubwa na mambo ya kisiasa badala ya kujielekeza katika taaluma ya elimu.

Kutokana na sera kama hizi, Kanisa linajikuta linakabiliwa na changamoto ya utoaji wa elimu bora na kwamba, kuna haja ya sauti ya kinabii kusikika kwa njia ya majadiliano yanayosimikwa katika ukweli, uwazi, ustawi na maendeleo ya watanzania katika sekta ya elimu. Tanzania haina budi kushinda kishawishi cha kuuza ubora wa elimu kwa kutafuta kura za watanzania!

Kuna haja ya kuwa na sera na miongozo ya kudumu, ili kuhakikisha kwamba, maboresho yanayokusudiwa katika sekta ya elimu yanazaa matunda muafaka na kwamba, wanafunzi wanaohitimu masomo yao nchini Tanzania wanaweza kukabiliana na ushindani kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Madhara ya kushuka kwa viwango cha ubora wa elimu nchini Tanzania yamejionesha hivi karibuni kwani ufaulu wa wanafunzi wanaopaswa kujiunga navyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania umeshuka sana na hivyo kuwa na idadi ndogo ya wanafunzi wanaopaswa kujiunga na elimu ya juu. Hizi ni changamoto za kibinadamu na kisiasa zaidi zinazokamisha mchakato wa maboresho ya sekta ya elimu nchini Tanzania.









All the contents on this site are copyrighted ©.