2014-08-20 12:06:05

Elimu ni ufunguo wa mageuzi ya kijamii nchini Madagascar


Kanisa Katoliki nchini Madagascar, limekuwa mstari wa mbele katika utoaji wa huduma za kijamii hasa katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Kanisa linapenda kuweka uwiano bora kati ya akili, tamaduni na kanuni maadili ili kuwasaidia wananchi wa Madagascar kupambana kikamilifu na changamoto za maisha. Ni changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Madagascar wakati walipofanya hija ya kitume mjini Vatican hivi karibuni.

Madagascar imebahatika kuwa na rasilimali nyingi ambazo kama zingeweza kutumika barabara, leo hii watu wake wangekuwa wamecharuka kwa maendeleo, lakini kwa bahati mbaya, wananchi wengi bado wanaendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini, magonjwa na njaa. Kinzani za kisiasa, kijamii na kiuchumi zimepelekea watu wengi kukosa matumaini ya kesho iliyo bora zaidi anasema Askofu Rosario Vella wa Jimbo Katoliki la Ambanja, lililoko Kaskazini mwa Madagascar.

Elimu makini ni njia pekee inayoweza kuwajengea uwezo wananchi wa Madascar kuweza kupambana na changamoto za maisha na hatimaye, kujipatia maisha bora zaidi. Kuna umati mkubwa wa watoto wadogo ambao wanapaswa kuwa darasani, lakini hawana nafasi hii, kiasi kwamba, kiwango cha watu wasiojua kusoma na kuandika nchini Madagascar kimefikia asilimia 31% ya wananchi wote wa Madagascar, hali ambayo inatisha na kuhuzunisha.

Hii inaonesha kwamba, jitihada za Umoja wa Mataifa kupambana na baa la ujinga kama sehemu ya mikakati ya utekelezaji wa Maendeleo ya Millenia zinakabiliwa na changamoto kubwa! Kiwango na ubora wa elimu inayotolewa nchini Madagascar ni cha hali ya chini kabisa. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, walimu wanaofundisha shuleni wana kiwango cha chini cha elimu.

Kanisa Katoliki limejipambanua kwa kuwaaandaa walimu kitaaluma na kimaadili ili waweze kutekeleza vyema wajibu wao ndani ya jamii na matokeo yake ni kwamba, shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki zinaonesha mafanikio makubwa katika sekta ya elimu. Wanafunzi wanaosoma katika shule na taasisi za elimu za Kanisa Katoliki licha ya kupatiwa ujuzi na maarifa, wanafundishwa pia misingi ya nidhamu, umuhimu wa familia, mshikamano na upendo wa kidugu na kwamba, utu na heshima ya binadamu vinapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza.

Haya ni mambo ambayo pia yamo katika maisha, mila na desturi njema za wananchi wa Madagascar, lakini kwa sasa yanaonekana kutoweka kama ndoto ya mchana! Kanisa Katoliki limeendelea kutoa huduma katika sekta ya afya kwa wote bila ubaguzi.

Tangu kuteuliwa kwake kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Ambanja kunako mwaka 2007, Askofu Vella alisoma alama za nyakati na kutambua kwamba, ujinga ndilo lililokuwa tatizo kubwa kwa waamini wake, kiasi kwamba, tangu wakati huo, akajielekeza kwa kuwekeza katika sekta ya elimu na leo hii amekwishajenga shule za msingi 50 zilizoenea vijijini.

Vijana wamemchangamotisha kujielekeza katika ujenzi wa Chuo kikuu na tayari Chuo kikuu cha Jimbo Katoliki la Ambanja kimezinduliwa mwaka 2014. Hapa vijana wamecharuka katika masomo kwani wanatambua kwamba, elimu ni ufunguo wa maisha kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Kitivo cha sheria kinaonekana kuwa na mvuto kwa wanafunzi wengi, ili kuimarisha utawala wa sheria na haki nchini humo, kwani mwelekeo wa sasa ni mwenye nguvu mpishe, vinginevyo utakiona cha mtema kuni!

Wananchi wa Madagascar wana imani na matumaini makubwa na Kanisa, kwani Kanisa limekuwa nao bega kwa bega wakati wa raha na shida, wakati wa kuomboleza na kucheka! Kanisa litaendelea kujielekeza katika kutafuta, kulinda na kutetea mafao ya wengi nchini Madagascar anasema Askofu Rosario Vella wa Jimbo Katoliki la Ambanja, Madagascar.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.