Papa akiwa safarini kurejea Roma alijibu dukuduku za wanahabari
Jumatatu, Baba Mtakatifu Francisko akiwa safarini kurejea Roma tokea Korea, alifanya
mkutano na wanahabari akiwa ndani ya ndege, kama fursa ya kujibu dukuduku za wanahabari.
Kati ya maswali yaliyoulizwa, ni maoni yake juu ya uwezekano wa kuunganisha
Korea Kaskazini na Korea Kusini, kuwa taifa moja, pia hali za vita vinavyoendelea
kusikika hapa na pale, hali ya Wakristo wachache wanaoteswa Iraq, safari ya Papa
Albania, Philadephia ... Sasa imekuwa kama ni jadi ya Mapapa wanapokuwa katika safari
ndefu za kimatiafa, kukutana na wanahabari ndani ya ndege , ambamo wanahabari hupata
muda wa kuuliza maswali mbalimbali. Na ndivyo ilikuwa wakati akitokea Korea. Swali
la kwanza,lililoulizwa lilitaka kujua Papa alilenga nini katika ukaribu wake na familia
za waathirika wa maafa ya feri iliyozama na maisha ya watu zaidi ya watu 300 kuangamia
Korea . Tukio lililokasirisha raia wengi wa Korea, kwamba, serikali haikutenda vyema.
Baba Matakatifu kwa heshima na hekima alijibu: "Wakati wa kupambana uso kwa
uso na maumivu na huzuni na majonzi, ni lazima kufanya kile moyo unachotamani kufanya"
Yeye alipata hisia kali za kuungana ana kwa ana na watu hao ktika maombolezo yao.
Lakini kwa kuwa haiwezekani kwake kufnaya hivyo ghafla, moyo wake ulimsukuma kumteua
Padre, amwakilishe katika maombolezo hayo. Na kwa namna hiyo, aliweza kujisikia
kuwa karibu zaidi na wateswa. Na kwamba, ukaribu huo, humpatia faraja, si ufumbuzi
wa janga, lakini kuwa pamoja na wateswa. Na alikumbuka, wakati alipokuwa Askofu Mkuu
wa Buenos Aires, aliweza kuwa karibu na waathirika wa majanga mawili ya kutisha lile
moto uliotokea katika ukumbi wa disco na kuua vijana 193, na ajali ya treni, iliyoua
watu 120. Na alizungumzia jinsi ilivyokuwa vigumu kwa mtu mwema, kutoendelea kuwa
na majonzi, wakati jamii iliyo kando yake bado inaomboleza.
Na akijibu swali
kuhusu mateso ya Wakristo na makundi ya watu wengine wachache wa dini nyingine, yanayo
sababishwa na watu wenye msimamo mkali wa utawala wa Kiislamu (ISIS), Papa alisema
kuwa ni halali kufanya kila linalowezekana kuzuia uchokozi na madhulumu hayo. Na alisisitiza
neno kusitisha akisema haina maana ya kutumia mabomu, lakini ni lazima kutathimini
vyema njia zote zinazolenga kusitisha madhulumu hayo , kwa lengo la kuzuia mauaji
zaidi. Na alikazia kwamba , katika matukio kama haya ya vita na madhulumu, tusisahau
kwamba , ni kwa mara ngapi kwa kisingizio cha kusitisha ukatili , mataifa yenye uwezo
wa kijeshi , yamepora mali za watu na hata kuongeza mauaji ya kivita kwa ajili ya
kujipatia ushindi. Papa anasema , katika vita hivi vya madhulumu, taifa moja peke
yake haliwezi kutoa maamuzi jinsi ya kuvishinda vita, na hivyo umoja wa Mataifa unakuwa
ni wajibu wake msingi , kuwa mahali pa majadiliano kwa ajili ya upatikanaji wa jawabu
sahihi la kusitisha madhulumu. Papa Francisco alieleza na kuonyesha kuwa Wakristo
wanaoteseka Iraki na kwingineko kwa sababu ya Imani yao kwa Kristo, wako katika
mtima wa moyo wake, na alisisitiza ukweli kwamba, Wakristo hao pamoja na makundi
mengine ya watu wachache wa imani mbalimbali, wanaokabiliana na mateso, na wao wote
wana haki sawa.
Paia alionyesha kuwa tayari wake wa kusafiri hadi Kurdistan,
kuungana na wakimbizi wanaokimbia madhulumu akisema ni jambo jema la kufanya. Na alitaja
mipango mbalimbali inayofanywa na Vatican akitoa mfano wa Kardinali Fernando Filoni
kutumwa Iraki, pia kuandika kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, na kuandika tamko
lake binafsi, lililotumwa kwa Manusio wote na serikali katika Mkoa wa Mashariki ya
Kati