2014-08-18 10:46:30

Zingatieni: taaluma, weledi, maadili na sheria za kazi!


Askofu Antony Crowley, Makamu mwenyekiti wa Tume ya Elimu, Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya amewataka wakuu wa shule kuhakikisha kwamba, wanatekeleza dhamana na wajibu wao kwa kuonesha uongozi bora unaojidhihirisha kwa kuwafahamu vyema wanafunzi wao pamoja na kuzingatia: taaluma, weledi na kanuni maadili na sheria za kazi.

Askofu Crowley, ameyasema haya hivi karibuni alipokuwa anazungumza na wakuu wa shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Kenya pamoja na wadau wengine katika sekta ya elimu. Wakuu wa shule wanapaswa kuwa ni kielelezo bora cha nidhamu, utendaji bora wa kazi kwa kutekeleza wajibu wao unaozingatia utu na heshima ya binadamu.

Umoja na mshikamano eneo la kazi ni mambo msingi katika maboresho ya sekta ya elimu. Walimu wajitahidi kuwafahamu wanafunzi wao barabara ili kuona mambo yanayokwamisha maendeleo yao kitaaluma na kutafuta mbinu za kuweza kupambana na vikwazo kama hivi. Wanafunzi waheshimiwe na kuthaminiwa, wapewe miongozo na malezi sahihi katika maisha yao, ili mwisho wa siku waweze kuwa ni raia wema.

Wakuu wa shule katika mkutano huu wamezindua pia Umoja wa Wakuu wa Shule za Kikatoliki, kwa ufupi CaSPA, kazi iliyofanywa na Askofu Maurice Muhatia Makumba, Mwenyekiti wa Tume ya elimu na mafundisho ya dini shuleni kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.